KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Wednesday, January 12, 2011

Afisa wa Congo akamatwa juu ya ubakaji

Maafisa na Umoja wa Mataifa umesema, serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo imemkamata afisa wa jeshi juu ya tuhuma za ubakaji wa raia wengi uliofanyika Januari 1 mashariki mwa nchi hiyo.

Lt Kanali Kibibi Mutware anashutumiwa kwa kuongoza ubakaji wa zaidi ya wanawake 50 huko Fizi, jimbo la Kivu ya kaskazini.

Kanali Kibibi ameyatupilia madai hayo na kusema ni uvumi.

Kumekuwa na matukio mengi ya ubakaji wa wanawake wengi mashariki mwa Congo, lakini hili limekuwa tukio kubwa la mara moja kutokea ambalo limehusisha jeshi.

Tahirou Diao, msemaji wa umoja wa mataifa huko Uvira karibu na Fizi, alisema maafisa wa kijeshi wa Congo walimkamata walipotembelea Fizi

Wanawake wa Congo wakipinga ubakaji


Maso'a Mwenembuka, mkuu wa manispaa ya Fizi, alithibitisha kumwona Kanali Kibibi akiwa amefungwa pingu na kuondoshwa, pamoja na takriban wanajeshi wengine 10 waliokamatwa wakihusishwa na ghasia hizo zilizotokea siku ya mwaka mpya.

Vyanzo vya kijeshi na mashirika ya kutetea haki za binadamu vimesema matukio hayo ya mwaka mpya yalianza wakati kundi la watu lilipomvamia askari ambaye alimpiga risasi raia- ikidaiwa kuwa walikuwa wakigombania mwanamke.

Baada ya hapo kundi la wanajeshi likaamua kulipiza kisasi kwa watu wa Fizi.

Ofisi ya umoja wa mataifa ilisema wanajeshi waliwapiga kisu watu 26, akiwemo mtoto mwenye umri wa miaka minne, kuharibu zaidi ya nyumba 200 na kubaka idadi kubwa ya wanawake.

Wakaazi wengi wa Fizi na muathirika wa madai hayo ya ubakaji wameshutumu Kanali Kibibi, afisa kamanda wa eneo hilo, kwa kuongoza vurugu hizo.

Lakini katika mahojiano na BBC wiki hii, alikana madai hayo na kusema wanajeshi waliofanya uhalifu huo walikiuka amri yake.

Ghasia za miaka 16 mashariki mwa Congo zimekithiri kwa udhalilishaji wa wanawake na watoto wa kike.

Zaidi ya wanawake 300, wanaume na watoto walibakwa na muungano wa makundi ya waasi katika mji wa Luvungi na vijiji jirani kaskazini mwa Kivu kilomita kadhaa kutoka kituo cha umoja wa mataifa mwezi Agosti

No comments:

Post a Comment