KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Thursday, December 2, 2010

Wanaodaiwa kupora maeneo waanza kujitokeza adharani


Nora Damian
SIKU moja baada ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka, kutangaza watu waliopora maeneo ya wazi kuyarudisha, mmiliki wa kiwanja kilicho jirani na Hoteli ya Palm Beach, kinachodaiwa kuwa ni cha wazi ameibuka hadharani na kusema anakimiliki kihalali.

Kiwanja hicho namba 1006 kilichoko Upanga jirani na Hoteli ya Palm Beach ni kati ya viwanja vinavyotajwa kuwa ni vya wazi.
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Taher Muccadam, alisema kiwanja hicho kilikuwa kinamilikiwa kwa hati namba 186164/25 iliyotolewa Januari Mosi, 1975.


Muccadam alisema kiwanja hicho namba 1006 kilichopo Upanga, jirani na Hoteli ya Palm Beach kilimilikishwa na Manispaa ya Ilala na miliki hiyo ilidumu miaka 99 kabla mwenyewe hajakinunua mwaka 2000.
Alisema alinunua kiwanja hicho kujenga jengo la ghorofa 22, lakini tangu wakati huo ameshindwa kuanza ujenzi kutokana na kuwepo kesi mbalimbali mahakamani kubishania kiwanja hicho.

Muccadam alisema mwaka 2000, kiwanja hicho kilifutwa kwa makosa, hivyo suala hilo lilipelekewa Mahakama Kuu na kufunguliwa kesi namba 70/2004 ambapo baadaye Wizara ya Ardhi ilipendekeza mgogoro umalizwe nje ya mahakama.
“Nashangaa kuona watu wanaobiashania kiwanja hiki walikuwa wapi tangu kesi ilipoanza mwaka 2004?” alihoji Muccadam.

Hata hivyo, Muccadam alisema wizara na Manispaa ya Ilala vilishindwa kutekeleza makubaliano hivyo ilimlazimu kufungua kesi nyingine Mahakama Kuu namba 107/2006.
Alisema aliendelea na malumbano hayo Mahakama Kuu kwa muda wote huo na hatimaye alishinda kesi na kurudishiwa kiwanja hicho na kwamba, mahakama ilikubali alipwe fidia ya dola 6 milioni za Marekani kama garama za ujenzi huo.

Mfanyabishara huyo alidai kuwa suala la kiwanja chake limekuwa likishikiwa bango na viongozi wachache wa serikali, ambao alidai wanashikizwa na mfanyabiashara anayeogopa ushindani.
Katika hatua nyingine, mfanyabiashara huyo amesema amefungua kesi Mahakama Kuu Kitengo cha Ardhi dhidi ya Mkurugenzi wa Mipango Miji, Wizara ya Ardhi na maofisa wenzake kwa kile alichodai kuwa wamedharau amri ya Mahakama Kuu.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Patrick Rutabanzibwa, alisema suala la kiwanja hicho wanalifuatilia na kwamba amri ya kusitishwa ujenzi huo tayari imetolewa

No comments:

Post a Comment