KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Wednesday, December 15, 2010

Muhimbili Wafanya Utafiti wa Chanjo ya Ukimwi


CHUO Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) kilichoko jijini Dar es Salaam, kinafanya utafiti mwingine wa chanjo ya virusi vya ukimwi (VVU) hapa nchini na Msumbiji.
Hayo yalielezwa juzi jijini Dar es Salaam na Makamu Mkuu wa Chuo cha
MUHAS, Profesa Kisali Pallangyo, mbele ya Rais Jakaya Kikwete wakati
wa mahafali ya nne ya chuo hicho yaliyofanyika katika eneo la chuo
hicho.

Alisema utafiti huo unajulikana kama Programu ya Utafiti wa Chanjo Dhidi ya VVU nchini Tanzania na Msumbiji (TaMoVac) na unafanywa chini
ya uongozi wa watafiti wa Chuo Kikuu Muhimbili na kwamba kwa sasa utafiti huo unaendelea.

Kwa mujibu wa Profesa Pallangyo matokeo ya utafiti huo ni mazuri na
yameleta msisimko kwa watafiti wa masuala ya chanjo dhidi ya VVU
duniani pote.

“…Hata hivyo napenda kusisitiza kwamba bado chanjo dhidi ya virusi vya
ukimwi haijapatikana kwa hiyo ni lazima kila mtu awe makini katika
kujikinga na maambukizi ya VVU,” alisema Profesa huyo.

Akizungumzia kuhusu utafiti wa chanjo ya majaribio dhidi ya VVU jijini
Dar es Salaam ulioanza mwaka 2007 Profesa Pallangyo alisema kazi ya
utoaji wa chanjo hiyo umekamilika tangu Julai mwaka huu.

Alisema kazi iliyopo kwa sasa ni kuona kama kinga hiyo itaweza kuua au
kupunguza kuzaliana kwa VVU.

“Kazi hiyo itafanyika kwa kuzihusisha maabara zetu. Aidha pamejengeka
uwezo wa kitaalamu nchini wa kuendelea na tafiti za aina hii,’ alisema
Profesa Pallangyo.

Alirudia kusisitiza kuwa matokeo ya utafiti huo wa awali yameonyesha
kuwa chanjo hiyo ni salama kwani hakukuwa na tukio lolote kubwa
lililotokea miongoni mwa washiriki 60.

“Chanjo hiyo imeweza kutengeneza vichocheo vya kinga dhidi ya VVU kwa
asilimia 100 kwa washiriki waliopatiwa chanjo zote tano. Haya ni matokeo mazuri sana kupitia hata matarajio ya watafiti wetu pia ni ya muhimu katika harakati za kutafuta chanjo dhidi ya VVU


Utafiti unaonyesha Wanaume Waoga Kupima VVU!!!



Muuguzi akitoa huduma kwa Mgonjwa mwenye VVU pamoja na TB.
Wanaume nchini wanadaiwa kuwa ndiyo waoga zaidi kupima Virusi vya Ukimwi (VVU) ukilinganisha na wanawake, huku wengi wao wakiishi kwa kutegemea zaidi majibu ya wake zao, utafiti umebaini.

Utafiti huo ambao umefanywa na Chama cha Waandishi wa Habari za Ukimwi (AJAAT), pia umegundua kuwa wanawake wengi ndiyo huambikizwa zaidi VVU ukilinganishwa na wanaume na hii yote ni kutokana na maumbile yao.

Meneja ufundi wa (AJAAT), Charles Kayoka, aliyasema hayo kwenye kampeni inayoendelea ya kuzuia maambukizi ya VVU kwa mama kwenda kwa mtoto.

Kampeni ya AJAAT)inadhaminiwa na Shirika lisilo la Kiserikali la Cepa pamoja na la Kimataifa la Global Aids Alliance.

Kayoka alisema katika utafiti wao kwenye baadhi ya mikoa nchini, wamegundua kuwa wanaume ni waoga mno kupima VVU na wakati mwingine hukataa kupima katika dakika za mwisho wakiwa hospitali na wake zao.

“Tulipata bahati ya kuwahoji wauguzi kwenye baadhi ya mikoa nchini, wakatuambia kuwa wanaokubali kupima kwa hiari yao Virusi vya Ukimwi wengi wao ni wanawake, lakini wanaume wamekuwa hawajitokezi kwa wingi,” alisema.

Aliongeza: “Tena walituambia wengine hufika hospitali wakiwa wameambatana na wake zao, lakini wamekuwa waoga kwa kuanza kupima na badala yake wanawatanguliza wake zao na baadaye hughairi na kudai kuwa majibu ya mkewe yatakuwa yametosha kabisa kujijua yeye yuko katika hali gani.”

Kayoka amewataka wanaume kuvaa ujasiri wa kiume wa kukubali kwa hiari yao kwani ni faida kwa familia nzima na taifa kwa ujumla.

“Ina maana wanaume wengi wanaishi kwa kutegema majibu wa wake zao, lakini hii si kweli kwa sababu mke anaweza kuwa hana mwanaume ukawa nao, au mkeo anao wewe huna, sasa hiyo itasaidia kuangalia mtaishi vipi ili mmoja wenu asiambuzwe,” alisema.

Pia, amesema utafiti huo umegundua kuwa wanawake ndiyo wanaoambukizwa zaidi virusi na hiyo yote hutokana na maumbile yao.

Aidha, amesema kuwa wanawake huambikizwa wakiwa katika umri mdogo kuliko wanaume na hiyo inatokana na kuwa umri wa kubalehe msichana ni mdogo kuliko mvulana, hivyo msichana huanza kujiingiza katika masuala ya mapenzi mapema

No comments:

Post a Comment