KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Thursday, December 2, 2010

Kawambwa awaahidi neema walimu, wastaafu


Sadick Mtulya na Fred Azzah

MAWAZIRI wapya wa serikali ya Rais Jakaya Kikwete wameendelea kutamba kwamba watashughulikia matikatizo yanayowakabili wananchi, huku Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Dk Shukuru Kawambwa akiahidi kuboresha masilahi ya walimu na wastaafu wa vyuo vya elimu ya juu vya umma.

Kawambwa Kawambwa alisema hayo jana wakati akizungumza na wafanyakazi wa wizara hiyokatika siku yake ya kuanza rasmi kazi.

Hata hivyo, Dk Kawambwa alisema kuwa atafanya kazi kimyakimya kama mchwa' na kuwataka wananchi kupima utendaji wake kwa matokeo ya kazi kwa sababu anaamini kuwa kazi inaweza kufanyika vizuri na mafanikio makubwa bila kutumia maneno makali.

Naye Waziri wa Mambo ya Ndani, Vuai Nahodha aliahidi kuwa nguvu zake atazielekeza zaidi kuwahudumia walalahoi na si wanaovaa suti na kutamba kuwa wananchi wamhukumu ndani ya miezi kulingana na ahadi yake na kuwahimizia watendaji katika wizara yake kuwa waadilifu.

Vuai ambaye alikuwa Waziri Kiongozi katika serikali ya awamu ya sita ya Zanzibar (SMZ), aliteuliwa katika nafasi hiyo, baada ya Rais Jakaya Kikwete kumteua kuwa mbunge alionya kuwa mtumishi yoyote atakayeshindwa kutekeleza ilani ya CCM ataadhibiwa.

“Utaratibu wangu wa utendaji utakuwa tofauti na wenzangu waliopita. Nataka ndani ya miezi sita wananchi wanihukumu kwa utendaji wangu pamoja na wizara kwa ujumla,’’ alisema Vuai.

Alifafanua kwamba msingi wa maneno yake hayo ni watendaji wa wizara hiyo kutoa huduma kwa kufuata sheria ipasavyo pamoja na kuheshimu maadili na miiko ya kazi.

Akizumgimaa kwa kutumia lugha ya tafsida na misemo mingi, Vuai alisema atafanya kazi usiku na mchana na kwamba hulka yake ni upole lakini hatokuwa tayari kuona utendaji mbovu.

Aliwaonya watendaji hao kuwa, watapata matatizo wasipotekeleza kivitendo Ilani ya CCM ya mwaka 2010/15, katika kusimamia amani na utulivu.

Katika kuhakikisha anafanikiwa katika mipango yake, Vuai alisema atalazimika kutembelea halmashauri zote pamoja na mabaraza ya usalama ya kata.

Naye Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Dk Shukuru Kwawambwa, ametaja vipaumbele vyake vinne atakavyofanyia kazi miaka mitano ijayo, huku akiibuka na msemo wa kufanya kazi kimya kimya kama mchwa kuwataka wananchi kumpima utendaji wake kwa matokeo ya kazi yake na siyo vinginevyo.

“Nilikuwa nasoma magazeti wanasema Kawambwa mpole na Naibu wake mwalimu, kweli wataiweza wizara ile… Nasema hatuhitaji kuwa wakali na kutetema cheche, mimi na watendaji nataka tufanye kazi kimya kimya kama mchwa na wananchi watupime kwa matokeo ya kazi yetu,” alisema Dk Kawambwa.

Kawambwa alisema baada ya uongozi wake katika wizara hiyo, anataka wananchi na vizazi vijavyo wamkumbuke kwa mambo makuu manne ambayo
ni kumaliza matatizo ya mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu.

Alisema katika kufanikisha hilo, atahakikisha mfumo wa utendaji wa bodi ya mikopo unafanyiwa kazi na kuwa, wanafunzi wanaostahili kupata mikopo hiyo wanaipata.

Alibainisha pia kuwa, chini ya uongozi wake atahakikisha wanatafuta njia za kutunisha mfuko wa fedha hizo za mikopo ili kutoa fursa kwa wanafunzi wengi zaidi kupata mikopo hiyo.

“Tunatumia fedha nyingi sana kwa ajili ya mikopo lakini bado haitoshi, kwa mwaka huu tuu Sh200 bilioni kwa asili ya mikopo, lakini hazitoshelezi mahitaji, lazima tuangalie njia nyingine za kutunisha mfuko huu ili wanafunzi wengi wapate mikopo kwa viwango wanavyostahili,” alisema Dk Kawambwa

Kipaumbele cha pili chake cha pili ni kuboresha maslahi ya wafanyakazi wa sekta elimu wakiwemo walimu, pamoja na wastaafu wa sekta hiyo.

Kipaumbele cha tatu ni kuboresha miundo mbinu katika taasisi za elimu, shule za sekondari na za msingi.

Alisema uboreshaji wa miundo mbinu ya majengo mbalimbali na mingineyo, utaenda sambamba na kuboreshaji wa vitendea kazi katika ngazi zote.

Alitaja kipaumbele cha nne kuwa ni kuboresha elimu kuanzia elimu ya msingi hadi ya juu tikaoenda sambamba na uimarishaji mitaala ya elimu ili iendane na mazingira, yawawezeshe wanafunzi kushindana ndani na nje ya nchi.

Alisema mambo hayo, ndiyo yeye na watendaji aliowataka kufanya kazi kimyakimya kama mchwa, ndiyo aliyowataka Watanzania wawapime kwa matokeo yake.

Juzi, Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(Tamisemi), George Mkuchika aliwataka wafanyakazi wa wizara hiyo, kutotoa siri za serikali na kwamba kufanya hivyo ni kinyume na maadili ya kazi.

"Nitakuwa mtii kwa taifa langu na kwa vyovyote vile sitotoa siri ya baraza la mawaziri, kiapo hiki tuliupa mawziri lakini ninyi(wafanyakazi wote) hata dereva kwa namna yoyote ile hampaswi kutoa siri za serikali,'' alisema Mkuchika.

Mkuchika ambaye pia ni naibu katibu mkuu wa CCM, alisema hata 'vimemo' kutoka ofisi moja kwenda nyingine havipaswi kuwekwa hadharani na kwamba vinatakiwa kuwa ni siri.

Wakati huo huo, Wakala wa Vitambulisho vya Taifa nchini (Nida) imesema vitambulisho vya taifa vitaanza kutolewa ifikapo mwezi Agosti, 2011.

Kaimu mkurugenzi wa Nida, Joseph Makani alisema mchakato wa kupata kampuni itakayochapisha vitambulisho hivyo, utakamilika Februari, 2011 na kwamba utangazaji rasmi wa zabuni utafanyika Desemba 8, 2010.

“Kila kitu kinakwenda vizuri, Desemba, 8 mwaka huu tutangaza rasmi zabuni. Februari, 2011 tutamtangza mshindi na Agosti, 2011 tutaanza rasmi kutoa vitambulisho vya taifa,’’ alisema Makani

No comments:

Post a Comment