KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Thursday, December 2, 2010

Kanisa Katoliki Sumbawanga bado tete


Mwandishi Wetu, Sumbawanga

SAKATA la mamia ya waumini wa Kanisa Katoliki Jimbo la Sumbawanga mkoani Rukwa kutengwa na wengine kufukuzwa waumini ndani ya kanisa hilo limezua sura mpya, kwa wakazi wa mkoa huo huku viongozi wa kanisa hilo wakivitaka vyombo vya habari kuwa makini wakati wa kutoa taarifa za suala hilo.


Kanisa hilo, limenukuliwa hivi karibuni kuwasimamisha waumini wake karibu kwa tuhuma za kuwapigia kura wagombea wa CCM ambao wanadaiwa kulidhalilisha kanisa hilo.
Aliyekuwa mgombea ubunge wa Jimbo la Sumbawanga kupitia CCM Aeshy Hillary pamoja na wagombea udiwani wa jimbo hili kwa nyakati tofauti wanadaiwa walisikika wakisema kuwa ukimchagua Rais Kikwete ni sawa na kumchagua Mungu’ Kikwete ni Mungu Baba na kwamba mbunge Aeshy ni Mungu Mwana huku madiwani wakifananishwa na mungu Roho Mtakatifu .

Hata hivyo habari za ndani ya kanisa hilo, zilieleza kuwa baadhi ya waandishi wanaoabudu katika kanisa hilo watachukuliwa hatua za kisheria kwa mujibu wa kanisa hilo wakituhumiwa kulifuatilia suala hilo wakati mapadri na waumini hawakutaka litangazwe.

Viongozi wa kanisa hilo, wanadaiwa kuendelea kupokea majina ya waumini kutoka kwa viongozi wa jumuiya ya watu wanaotakiwa kutengwa na kanisa hilo.

Baadhi ya wakazi wa hapa walianza kupata hofu dhidi ya waandishi wanaofuatilia sakata hilo na kusema kuwa wasipokuwa makini wanaweza kupata uendawazimu kutokana na maombi yanayofanywa na waumini wa kanisa hilo.

Katika kipindi cha kampeni za uchaguzi mkuu, baadhi ya waumini hao, waliotengwa wanadaiwa kuwafafanisha wagombea ubunge na Urais kupitia CCM na utatu mtakatifu

Hata hivyo waumini na wananchi wa Mji wa Sumbawanga wamemtuhumu aliyekuwa mgombea ubunge wa jimbo hilo kupitia CCM Hillary pamoja na wagombea udiwani wa jimbo hilo kwa kuzusha tafrani hiyo.

Kwa mujibu wa vyanzo vya habari inafafanua kuwa kauli hiyo ilitolewa vibaya na baadhi ya waumini wa dini hiyo huku wengine wakitilia mkazo kuwa ni kweli mbunge huyo alitamka hadharani akiwa katika mkutano wake wa kampeni uliofanyika Izia mjini Sumbawanga.

Chanzo kimoja cha habari kinaeleza aliyekuwa mgombea ubunge huyo, alifafananisha utatu huo mtakatifu na mafiga matatu kauli inayotumiwa na wanachama wa CCM kwamba ili kauli hiyo itimie ni lazima awepo diwani ,mbunge na rais.

Kutokana na hali hiyo, mbunge huyo, alinukuliwa akisema kwamba katika vitabu vitakatifu kuna utatu mtakatifu na katika siasa kuna mafiga matatu na kusema kuwa kauli hiyo ilikuwa ni kauli ya kuwavuta wananchi ili waweze kumpatia kura za ndio katika uchaguzi mkuu uliopita wa Octoba mwaka huu.

Vyanzo hivyo vya habari vinaeleza kuwa kauli hiyo ilionekana kuwaudhi viongozi na waumini wa makanisa ya kikatoliki katika jimbo hilo la Sumbawanga.

Katika kipindi cha wiki ya mwisho ya kampeni mgombea huyo alionekana akiomba radhi katika mikutano yake ya kampeni na kusema kuwa yeye hakuwa na lengo wala nia mbaya ya kufafanisha mafiga matatu na utatu mtakatifu.

Waziri Mkuu Mizengo Pinda aliyefika katika mkutano wa kampeni uliofanyika katika kiwanja cha Shule ya Sekondari Msakila, aliwaomba radhi wananchi kutokana na kauli hiyo

No comments:

Post a Comment