KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Thursday, December 2, 2010

‘Fanyeni utafiti kabla ya kuanzisha biashara’


WANAWAKE nchini wameshauriwa kujikita katika suala la ujasiriamali ili
kujikomboa katika umaskini.
Wametakiwa pia kufanya utafiti madhubuti kabla ya kuanzisha biashara ili kuweza kuepukana na mambo yanayoweza kuwa vikwazo katika biashara zao.

Ushauri huo umetolewa na mkufunzi wa semina ya ujasiriamali Hamisi
Mpinga, katika Chuo cha Uandishi wa Habari na Utangazaji Arusha (AJTC).

Mpinga alisema kuwa, wanawake wanatakiwa kutambua uwezo wao katika biashara na si kukata tamaa na kuendelea kudidimizwa na umaskini.

Alisema kuwa, wanawake wengi nchini wamekuwa wakishindwa kujihusisha
na biashara ndogondogo kutokana na kutojiamini.

“Wanawake wengi wamekuwa wakionyesha hali ya woga, wasiwasi na hawajiamini kama wanaweza kufanya kitu jambo ambalo si sahihi” alisema Mpinga.

Alisema kuwa, wanawake wanatakiwa kuonyesha uwezo walio nao kifikra na
kiutendaji ili kuweza kuondoa dhana potofu iliyojengeka miongoni mwa
Watanzania kuwa mwanamke hana uwezo wa kumiliki biashara.

“Ili mwanamke ajikite katika suala la ujasiriamali ni lazama awe na uwezo wa kutambua vyanzo mbalimbali vya biashara hatua itakayowawezesha kuwainua kiuchumi ikiwa ni pamoja na kufanya utafiti madhubuti kabla ya kuanzisha biashara ili kuweza kuepukana na mambo mbalimbali ambayo ambayo yanaweza kuleta vikwazo katika biashara” alisema.

Alisema kuwa, utafiti ni kitu muhimu wakati unapohitaji kuanzisha
biashara yeyote kama kubwa au ndogo kwani husaidia kuepuka vikwazo visivyo na umuhimu.

Pia alitaja changamoto zinazowakabili wanawake katika kujihusisha na suala la ujasiriamali kuwa ni pamoja na ukosefu wa mitaji, elimu pamoja na ukosefu wa ushirikiano katika familia zao.

Changamoto nyingine ni pamoja na mfumo dume, kukata tamaa kukosa fursa ya kujieleza , kukosa ushauri mzuri wa biashara pamoja na kutojiamini

No comments:

Post a Comment