KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Thursday, December 30, 2010

HOJA YA KATIBA: CUF wataka Werema, Kombani wafutwe kazi


CHAMA Cha Wananchi (CUF), kimemshauri Rais Jakaya Kikwete, kuwafukuza Waziri wa Sheria na Mambo ya Katiba Celina Kombani na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Jaji Frederick Werema kutokana na kuwachanganya Watanzania kuhusu suala la Katiba.

Mbali na ushauri huo chama hicho pia kimeeleza kuwa kauli za watendaji hao wa serikali zimesababisha hata kauli ya Rais aliyoitoa Desemba 31 mwaka huu, kuhusu suala hilo ionekane ina utata na hivyo kuitaka Ikulu kuondoa utata huo kwa kuifafanua zaidi.

Hayo yalielezwa jana na Kaimu Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Julius Mtatiro alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari Makao Makuu ya chama hicho jijini Dar es Salaam.

Mapema mwezi ulipo, wakati mjadala wa Katiba ukiwa

umepamba moto, Kombani ambaye ndiye waziri mwenye dhamana akitoa maoni yake juu ya suala la katiba mpya alisema haoni umuhimu wa suala hilo sasa na kufafanua kwamba serikali haina bajeti yake.

"Katiba mpya kwa sasa haiwezekani kabisa kwani sio muhimu na kuwa serikali haina bajeti ya kushughulikia katiba mpya," alisema Kombani. Naye Mwanasheria Mkuu wa Serikali Frederick Werema, alisema "Kuandika Katiba mpya hapana, lakini kufanya marekebisho kwa kuondoa au kuongeza mambo fulani kwenye katiba, ruksa.”

Jaji Werema alisema hayo Desemba 27 mwaka jana alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari Ikulu jijini Dar es Salaam baada ya kumalizika kwa hafla ya kumwapisha Jaji Mkuu Mpya, Jaji Mohamed Othman Chande.

"Suala la kubadilisha ibara zinazoonekana kutokidhi haja na kuingiza mambo mapya kwenye katiba, linakubalika na kwamba hayo yamekuwa yakifanyika," alisisitiza Jaji Werema na kutolea mfano mabadiliko ya katiba yaliyoruhusu kuingizwa kwa haki za binadamu.

Werema alisema “Lakini si kila mtu analolisema lifuatwe. Tukisema kila mtu anachokisema tukifuate haitakuwa sawa. Kwa mfano mimi kule kwetu wafugaji nao watataka mambo ya ng’ombe wao yaingizwe kwenye katiba, na Wahaya pia wanaweza kusema tuingize kwenye katiba ndizi zao, hii si sawa;” alisisitiza Jaji Werema.

Jana akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Mtatiro kutokana na watendaji hao kupingana kwa kauli, CUF inamtaka Rais Kikwete kuwapumzisha Kombani na Werema walioonekana kuropoka mambo ya kuwakatisha tamaa Watanzania kuhusu suala hilo.

"Kama Rais Kikwete atakuwa makini, anapaswa sasa kuwapumzisha Kombani na Werema ili wasiendelee kutia doa jeusi serikali yake ambayo tayari imejaa kila aina ya matatizo," alisema Mtatiro.

"Kombani alisema katiba mpya kwa sasa haiwezekani na siyo muhimu, lakini pia serikali haina bajeti ya kushughulikia suala hilo, Jaji Werema alisisitiza kwa nguvu zote kwamba katiba mpya haiwezekani na akasema kitakachofanyika ni kuiwekea viraka katiba hii, iliyotoboka na Rais sasa anasema ataanzisha mchakato wa kuitazama upya katiba ya nchi kwa lengo la kuihuisha. Huku ni kutuchanganya," alisema Mtatiro.

Aliendelea "CUF tunasema wanatuchanganya kwa kuwa kwa kauli hizo za Kombani na Werema, kauli ya Rais pia sasa ina utata kwani naye hakutaka kueleza anasimamia lipi kati ya kuiwekea viraka katiba iliyopo au kuandika katiba mpya." Aliendelea "Katika mambo hayo ya katiba, watu wake wakubwa na wataalamu ni hao, sasa inapotokea wanatofautiana kimsimamo hadharani halafu rais naye anakuja na msimamo wake, ni tatizo kubwa linalohitaji ufumbuzi wa kina," alisema Mtatiro.

Mtatiro alibainisha kuwa CUF itapingana na juhudi zozote za serikali kuunda Kamati ya Marekebisho ya Katiba itakayoenda kufanya kazi ya kutia viraka katika katiba iliyopo, kwani lengo la Watanzania si marekebisho ya katiba bali kuandikwa katiba mpya.

"Kama kauli ya rais Kikwete inaamanisha kutaka iundwe katiba mpya, CUF inamuunga mkono, lakini kama anataka kuifanyie marekebisho katiba iliyopo, hatutashirikiana naye," alisema.

35555898**/*/7Akinukuu hotuba ya Rais Kikwete, inayosema “jambo la nne ambalo tulilo kubaliana kufanya ni kuanzisha machakato wa kuitazama upya katiba ya nchi yetu kwani lengo la kuihuisha ili hatimaye tuwe na katiba inayoendana na taifa lenye umri wa nusu karne,” Mtatiro alisema, rais hakueleza bayana nini anachotaka kifanyike.
Wakati Jitihada za kumpata waziri Kombani kuzungumzia msimamo huo wa CUF zikigonga mwamba jana, Jaji Werema aliwahi kuliambia gazeti hili kuwa "Sijiuzulu ng'o." kwa kauli hizo.

Alisema ''Wanaotaka nijiuzulu ni wale wasiofikiria, kwani kila mtu ana nafasi yake ya kuongea kuhusu katiba. Mimi nimetoa mawazo yangu na wengine wakitaka watoe ya kwao," alisema Werema. Aliendelea, ''Kunitaka nijiuzulu ni fikra za kichanga sana na potofu. Mtu mwenye upeo mpana hawezi kusema Mwanasheria Mkuu ajiuzulu kwa hili,"alisema
Julius Mtatiro, Kama Rais Kikwete atakuwa makini, anapaswa sasa kuwapumzisha Kombani na Werema ili wasiendelee kutia doa jeusi Seriakli yake

No comments:

Post a Comment