KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Friday, November 19, 2010

Gambia yafukuza maafisa ubalozi wa Iran


Gambia imesema inakatisha uhusiano wake na Iran, na kuwataka wawakilishi wote wa serikali ya Iran waliopo Gambia kuondoka katika kipindi cha saa 48.

Maafisa wa taifa hilo dogo la Afrika Magharibi, hawajatoa sababu ya kuchukua hatua hiyo.

Hata hivyo, mwezi uliopita Nigeria ilisema imekamata shehena ya silaha zinazosafirishwa kinyume cha sheria, ambazo inadaiwa zilikuwa zikipelekwa nchini Gambia.

Shinikizo

Afisa wa ngazi ya juu wa Iran Alaeddin Borujerdi amesema hatua hiyo ya Gambia imechukuliwa kutokana na shinikizo kutoka Marekani.

Mamlaka za Nigeria zilisema zilikamata silaha hizo zikiwemo mabomu ya kurushwa na roketi na mabomu ya kurushwa kwa mkono,zikiwa katika makontena yaliyoandikwa kuwa yana vifaa vya ujenzi

Silaha zilizokamatwa Nigeria


Kampuni ya usafirishaji wa majini ya Ufaransa CMA CGM, ambayo ilisafirisha shehena hiyo, imesema zilifanywa juhudi za kuipeleka meli yake nchini Gambia, kabla ya polisi wa NIgeria kuikamata.

Vikwazo

Shirika rasmi la habari la Iran IRNA limeripoti kuwa Bw Borujerdi, ambaye ni mwenyekiti wa kamati ya Usalama wa Taifa na Sera za Kimataifa wa bunge la Iran, amethibitisha kuwa kampuni binafsi ya Iran ilipeleka silaha nchini Gambia, lakini alisema silaha hizo zilikuwa zimefuata "utaratibu wote wa kanuni za kimataifa".


Nigeria imeishitaki Iran katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kufuatia kukamatwa kwa silaha hizo.

Iran imewekewa vikwazo na Umoja wa Mataifa kwa sababu ya mipango yake ya nyuklia na imepigwa marufuku kuuza, au kusafirisha silaha

No comments:

Post a Comment