KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Wednesday, October 13, 2010

Kesi ya Ghailani yasikilizwa Marekani



Ahmed Ghailani


Waendesha mashataka walisema, aliyekuwa mfungwa wa Guantanamo anayehusishwa na mlipuko wa mabomu katika ubalozi wa Marekani nchini Tanzania alikuwa ni mmoja wa kundi la al-Qaeda aliyedhamiria kuwaua Wamarekani.

Kwenye taarifa za ufunguzi katika kesi ya Ahmed Khalfan Ghailani, waendesha mashtaka walisema alinunua lori na matenki ya gesi yaliyotumika kwenye shambulio la Dar es Salaam la mwaka 1998.

Mshtakiwa amekana kuisaidia al-Qaeda na kuua watu 224 katika milipuko miwili ya mabomu.

Bw Ghailani ni mfungwa wa kwanza wa Guantanamo Bay kukabiliana na kesi ya kiraia.

Mwendesha mashtaka Nicholas Lewin alisema, " Mshtakiwa aliyafanya yote hayo -kwasababu alikusudia kutimiza lengo la al-Qaeda, kuua Wamarekani."

Bw Lewin aliiambia jopo la mahakama watasikia ushahidi kutoka kwa aliyekuwa "mtoa taarifa" wa al-Qaeda, ambaye amekiri makosa.

Alisema baadhi ya watu walionusurika kwenye milipuko hiyo watatoa ushahidi.




Ahmed Ghailani akiwa mahakamani



Bw Lewin alisema baada ya Bw Ghailani kwenda Pakistan, "hakudhania kuwa ipo siku atakabiliana na mashahidi wote hao- hapa katika mahakama hii ya Marekani".

Wakili wa utetezi Steve Zissou amemwelezea Ghailani kama mtu "aliyelaghaiwa" kwa ajili ya al-Qaeda na alikuwa akitumwa na marafiki ambao yeye alidhani ni wafanyabiashara , na si magaidi.

Bw Zissou alisema, tofauti na wengine wanaohusishwa na milipuko hiyo ya mabomu, Bw Ghailani hakwenda katika makambi ya mafunzo na hakutiwa kasumba yeyote.

Wakili alisema, " Si mfuasi wa al-Qaeda na wala hakuwa na malengo sawa na kundi hilo."

Uongozi wa Obama una matumaini ya kusikiliza kesi kama hizo za kiraia kwa wafungwa wengine muhimu wa Guantanamo.

Inaweza pia kumhusisha anayedaiwa kuwa mwandaaji mkuu wa mabomu ya Septemba 11, Khalid Sheikh Mohammed.

Lakini waandishi wanasema kesi imeanza kuwa na utata baada ya uamuzi wa jaji Lewis Kaplan alioutoa wiki iliyopita wa kuukataa ushahidi kutoka upande wa mwendesha mashtaka katika kesi ya Ghailani.

Shahidi huyo, Hussein Abebe, alitarajiwa kutoa ushahidi kuwa aliuza milipuko ya TNT iliyotumika kwenye milipuko ya mabomu ya ubalozi wa Marekani kwenye mji wa Dar es Salaam, Tanzania kwa Bw Ghailani Agosti, 1998.

Lakini wiki iliyopita jaji huyo alitoa uamuzi kuwa shahidi huyo hawezi kutoa ushahidi kwani alitajwa na Bw Ghailani huku akiwa "anapewa vitisho."

No comments:

Post a Comment