KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Monday, August 9, 2010

Rais mpya wa Colombia ahimiza maridhiano


Juan Manuel Santos ameapishwa kuwa rais wa 40 wa Colombia katika sherehe zilizohudhuriwa na viongozi wengi kutoka eneo la Latin America.

Kwa mshangao mkubwa, katika sherehe hizo zilizofanyika mjini Bogota, Rais Santos alitoa hotuba inayohimiza maridhiano.

Akifahamika kama waziri wa ulinzi mwenye msimamo mkali wakati wa rais anayeondoka madarakani Alvaro Uribe, Santos alisema "neno vita halipo katika kamusi yangu".

Ujumbe huu haukuwa mahsusi kwa waasi wanaofuata sera za Kimarxist,ambao wamekuwa wakipigana kwa miaka 46 kwa lengo la kuipindua serikali, bali hata kwa majirani wa Colombia, haswa Venezuela na Ecuador, ambazo hazina uhusiano na nchi yake.

Hatua aliyochukua Rais Santos ibi tofauti na ile ya mtangulizi wake, Bw Uribe, ambaye alikuwa na mazoea ya kutoa matamshi makali dhidi ya waasi.

Rais Santos alieleza kuwa huenda akawa tayari kufanya majadiliano na waasi , akisema "mlango wa mazungumzo haujafungwa".

Santos anaingia madarakani akiungwa mkono kwa asilimia kubwa ya bunge, hali ambayo inaweza kumpa fursa ya kurekebisha uhusiano na majirani zake.

Hata hivyo serikali inakabiliwa na changamoto kubwa kutoka kwa waasi wenye kiasi cha wapiganaji 10,000 wenye nguvu, wakiwa na ushirikiano na magenge ya madawa ya kulevya, huku nchi ikibakia katika vita vya wenyewe kwa wenyewe kwa miaka 46 sasa.

Rais wa Venezuela, Hugo Chavez, amewakilishwa na waziri wake wa mambo ya nje katika sherehe hizo.

Bw Chavez alivunja uhusiano na Colombia wiki mbili zilizopita, baada ya utawala wa mjini Bogota kumshutumu kuwapa hifadhi waasi wa kundi la FARC la Colombia.

Chavez pia alimwomba Rais wa Brazil, Luiz Inacio Lula da Silva, ambaye amekuwa akijaribu kutatua mzozo kati yan nchi hizo mbili, kuwasilisha salamu kwa rais huyo mpya wa Colombia, Bw Santos.

No comments:

Post a Comment