KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Friday, June 18, 2010

Benki ya Exim yatoa vitanda vya wajawazito Mbeya

Benki ya Exim leo ilitoa vitanda vinane vyenye thamani ya Shilingi Milioni 8.5 kwa ajiri ya kujifungulia wanawake wajawazito katika mkoa wa Mbeya.
Akikabidhi vitanda hivyo Mkurugenzi Mkuu wa benki hiyo, Sabetha Mwambenja alisema benki yake inatoa vitanda hivyo ikiwa ni jitihada zake za kuboresha maisha ya wanawake na Watanzania wote kwa ujumla

“Tunatambua umuhimu wa afya za akina mama na ndiyo maana tumeguswa na tatizo hili mkoani Mbeya na kuamua kushirikiana na Mkoa ili kuboresha afya za akina mama,”

Mwambenja alisema kuwa msaada huo ni muhimu sana katika kuhakikisha kwamba wakazi wa Mbeya wanapata huduma bora za afya.

“Tutaendelea kushirikiana kila mara si kwa Mbeya peke yake ila hata kwa maeneo mbalimbali ya nchi lengo ni kuhakikisha kwamba Watanzania wanapata huduma bora za afya".

Naye katibu tawala mkoa wa Mbeya, Bertha Swai, akipokea msaada huo alisema kwamba msaada huo ni muhimu sana kwa hospitali za mkoa wake kutokana na mahitaji ya vitanda hivyo.

Alisema vitanda hivyo vitagawiwa kwa Wilaya nane za Mkoa wa Mbeya.

Alisema kwa wastani katika mkoa wake kitanda kimoja kinatumika kwa akina mama 20 na kwamba kwa mwezi mmoja kitanda kimoja kinaweza kutumiwa na akina mama 9000 wakati kwa mwaka wastani wa akina 72,000 wanatumia kitanda kimoja.

“Hivyo mnaona ni jinsi gani msaada huu kutoka Exim ulivyo muhimu sana kwetu” alisema

Alisema serikali inafarijika inapoona sekta binafsi ikijiendesha kwa tija na hatimaye kushirikiana na serikali katika kuboresha huduma za jamii.

Aliipongeza benki ya Exim kwa msaada huo na kuzitaka taasisi nyingine kuiga mfano wake.

Benki ya Exim ni miongoni mwa benki zinazokua kwa kasi ikiwa na matawi 18 nchini kote inatoa huduma mbalimbali za kibenki, ikiwa na kitengo maalum cha mikopo ya wanawake.

No comments:

Post a Comment