KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Monday, May 24, 2010

Kasri ya Rais wa Somalia yashambuliwa


Wapiganaji wa al-Shabab wamerusha mabomu katika kasri ya Rais wa Somalia, vilivyochochea mapigano makali yaliyosababisha mauaji ya takriban watu 14.

Majeshi ya serikali, yanayoungwa mkono na majeshi ya usalama ya Umoja wa Afrika, yalijibu mashambulio hayo ili kulizuia kundi hilo lililoshawishiwa na al-Qaeda mjini Mogadishu.

Rais Sheikh Sharif Ahmed hakuwa ndani ya jengo hilo wakati wa shambulio hilo, kwani alikuwa Uturuki kwenye mkutano wa amani.
Serikali yake inayoungwa mkono na Umoja wa Mataifa inadhibiti maeneo machache ya taifa hilo lenye mgogoro.

Wapiganaji wameshambulia wilaya za Shibis na Bondhere kaskazini mwa mji mkuu, na kusababisha mapigano makali.

Raia mmoja wa Mogadishu aliyeshuhudia miili kadhaa amesema miongoni mwa waliofariki dunia ni watu watano wa familia moja waliouawa bomu lilipotua kwenye nyumba yao.

Msemaji wa jeshi la Umoja wa Afrika AU, ameteta uamuzi wake wa kujilinda dhidi ya wanamgambo.

Meja Barigye Ba-hoku, " Watu wanatakiwa kuelewa makubaliano yetu ni nini- tuko hapa kulinda mashirika ya kiserikali ya Somalia na pia tuna mipaka."

Katika mkutano huko Istanbul, katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon amewasihi wafadhili kuunga mkono serikali ya Rais Ahmed.

Somalia imekumbwa na vurugu kwa zaidi ya miongo miwili na maelfu ya watu wamekimbia makazi yao.

Al-Shabab na makundi mengine ya kiislamu yanadhibiti maeneo mengi ya kati na kusini mwa Somalia.

No comments:

Post a Comment