KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Thursday, May 6, 2010

Bayern Munich watawazwa mabingwa Ujerumani.


Chelsea na Manchester United kuamua mzizi wa fitina Jumapili ijayo.

MICHEZO MWISHONI MWA WIKI:

Louis van Gaal,kocha wa mabingwa wapya wa Ujerumani-Bundesliga, ameahidi kusherehekea kupita kiasi Jumamosi ijayo, siku Bayern Munich itakapokabidhiwa Kombe la ligi mwishoni mwa msimu huu.Chelsea na manchester united zitaamua nazo Jumapili ijayo nani ni bingwa mpya na wa zamani wa Premier League.

Na huko Spain ,La Liga, mreno Cristiano Ronaldo ,amefufua matumaini ya Real ya kuivua taji FC Barcelona ,ingawa Barca imetamba kwa mabao 4-1 dhidi ya Villarreal.

Kocha wa Bafana Bafana,Carlos Parreira, ametangaza kikosi chake cha muda kwa changamoto za Kombe la dunia. Tutawachukua pia Afrika Mashariki tukisikia mapya kutoka viwanja vya michezo nchini Tanzania na Kenya.

Bayern Munich tayari, imeshatawazwa nmabingwa wa Ujerumani msimu huu baada ya kuizaba Bochum Jumamosi, mabao 3:1 .Mahasdimu wao wakubwa katika kinyan'ganyiro cha taji la ubingwa-Schalke, kwaliteleza walipo chapwa nyumbani mabao 2:0 na Werder Bremen.

Jumamosi ijayo, siku ya mwisho ya Bundesliga, Bayern Munich itacheza na timu ya mkiani Hertha Berlin, ambayo imesha teremshwa daraja ya pili baada ya kumudu sare na Leverkusen juzi.Munich inaania vikombe 3 msimu huu-viwili nyumbani na kimoja nje-champions league.Mei 22,Munich itapambana na Inter Milan katika finali ya kombe la klabu bingwa la ulaya.Tayari kocha wa Munich, Louis van Gaal, anasema anajiandaa kwa sherehe kubwa:Kuhusu kushindwa kwa mpinzani wake Schalke,alisema:

"Nilitarajia kuwa Schalke haingeshinda na jioni hii nina furaha kubwa."

Nae kocha wa Schalke ,Felix Magath aliekosea kidogo tu kuitawaza Schalke mabingwa baada ya msimu uliopita kuivalisha taji Wolfsburg alisema,

"Nimeridhika mno kupata nafasi ya kucheza champions league msimu ujao -jambo ambalo hakuna alietazamia na hata mimi binafsi."alisema Felix Magath.

Ama katika Premier League-Ligi ya Uingereza,uamuzi na mzizi wa fitina kati ya Chelsea na Manchester United utakatwa Jumapili ijayo.Mwishoni mwa wiki Chelsea inayoongoza Ligi, iliilaza Liverpool kwa mabao 2:0 wakati Manu ilitimua nje Sunderland kwa bao 1:0.

Afrika Kusini-Bafana Bafana, ndio itakayofungua dimba la Kombe la dunia na Mexico hapo Juni 11 na swali ni je, wenyeji hawa watatamba nyumbani alao wasije kuwa wenyeji wa kwanza katika historia ya Kombe la dunia kuaga mashindano duru ya kwanza ?

Kuepusha msiba kama huo, kocha wa Bafana bafana, mbrazil, Carlos Parreira,alitangaza mwishoni mwa wiki kikosi chake kisicho cha mwisho kwa Kombe la dunia:

Kama ilivyotarajiwa, Parreira alieitawaza Brazil, mabingwa wa dunia, 1994 nchini Marekani, amewachagua wachezaji kadhaa wa afrika Kusini wanaocheza dimba nchi za n'gambo.Lakini hakuna hata mmoja aliekuwamo katika kile kikosi kilichopiga kambi yake kwa mazowezi huko Brazil au Ujerumani mwezi uliopita.

Taarifa iliotolewa na Shirikisho la Dimba la Afrika Kusini (SAFA), Parreira amesema kuwa, amewateua wachezaji wengi kwavile, hana uhakika ,lini wachezaji wa kigeni watakuwa na nafasi ya kuichezea timu ya Taifa.Kwani, Bafana Bafana, tayari ina miadi 2 mwezi huu:Mei 16 na Mei 24.FIFA-Shirikisho la dimba la dunia, limeweka sheria kuwa ni kuanzia Mei 23 wachezaji wote waruhusiwe kujiunga na timu zao za taifa na sio kabla:

Isitoshe, hajui wachezaji hao watawasili wakiwa hali gani-fit au si fit.Baadhi yao, anasema, wamecheza mechi nyingi mno kama vile Steven Pienaar wakati wengine wamecheza mpambano 1 au 2 tu.

"Maarifa ni muhimu sana na natumai yatasaidia yataimarisha uwezo wa kiufundi wa timu yetu." -alisema Parreira.

Mchezaji alieingizwa bila ya kutarajiwa katika kikosi hicho cha wachezaji 29 kwa Kombe la dunia ni kipa anaecheza Ujerumani, Rowan Fernandez,ambae tangu Januari, mwaka huu hakucheza dimba kwavile, aliumia.Parreira amesema amemchagua Fernandez ,ili kuwa mmoja kati ya makipa 4 ili kujua alivyo fit.

Kikosi cha Bafana Bafana, kilichoteuliwa kinajumuisha kikosi cha wachezaji wa Premier League-ligi ya Uingereza kama vile Pienaar kutoka Everton na nahodha Aaron .Bafana Bafana ilishinda mpambano wake wa juzi na Jamaica,kabla haikurejea nyumbani kutoka kambi yake nchini Ujerumani.

Mojawapo ya timu 32 zitakazoania Kombe la Dunia, nchini Afrika Kusini, ni Korea ya Kaskazini. Kikosi cha Korea ya kaskazini , kinapanga kupiga kambi yake ya mazowezi nchi jirani ya Zimbabwe.Waziri wa utalii wa Zimbabwe amearifu kwamba, timu ya Korea ya kaskazini inapanga kufanya mazowezi yake katika Uwanja wa mpira wa Harare mwezi ujao kabla kuanza Kombe la dunia. Hapo awali, timu hiyo ilikuwa ifanye mazowezi yake mkoani Matabeleland.

Chama cha Upinzani cha ZAPU-Zimbabwe African People's Union , kilipanga kuandamana kupinga Korea ya kaskazini kufanya mazowezi Zimbabwe.Kisa nini ?

Chama hicho cha ZAPU kinadai wakaazi wa mkoa wa Matabeleland hawakuwasamehe wakorea ya kaskazini, kwa kuwapa mafunzo wanajeshi wa Zimbabwe, ili kukandamiza uasi miaka ya 1980.Raia alfu kadhaa waliuwawa huko Matabeleland.Kwahivyo, alao kwa wakaazi wa Matabele, Korea kaskazini , haikaribishwi Zimbabwe.

Waziri wa utalii wa Zimbabwe, Walter Mzembi,amekanusha kubadilishwa kituo cha mazowezi kutoka kambi ya awali huko Matabeleland na kuhamishiwa mji mkuu Harare.

Tukibakia katika medani ya kabumbu barani Afrika, huko Afrika Mashariki pia Taifa Stars-Tanzania ilikuwa uwanjani na jirani zao rwanda mjini Dar-es-salaam,lakini waliagana kwa bao 1:1 kwa mabao ya Mrisho N gasa na Roger Tchouassi.Katika kinyan'ganyiro cha kombe la vijana duru ya kwanza,Tanzania ilitamba kwa mabao 3:1 la Malawi.

Mwandishi: Ramadhan Ali/RTRE/AFPE

Uhariri: Abdul-Rahman

No comments:

Post a Comment