KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Friday, May 21, 2010

Aston Villa yakataa kumuuza James Milner

Aston Villa imekataa zabuni ya Manchester City ya paundi milioni 20 kumnunua mchezaji wao wa kimataifa anayechezea timu ya taifa ya England James Milner.


Aston Villa yakataa kumuuza James Milner

Msemaji wa Villa amesema "Tumepokea maombi kutoka Manchester City ya kumnunua James Milner na hilo tumelikataa."

"Tunapanga kukaa chini na James pamoja na mwakilishi wake baada ya fainali za Kombe la Dunia ili kuafikiana mkataba mpya wa muda mrefu na huo ndio msimamo wetu."

Kiungo huyo mwenye umri wa miaka 24 hivi karibuni alishinda tuzo ya mchezaji wa mwaka kijana kutoka Chama cha Wacheza soka wa Kulipwa- PFA.

Milner mzaliwa wa Leeds alijiunga na Aston Villa mwaka 2008 kwa kitita cha paundi milioni 12 kutoka klabu ya Newcastle, kwa wakati huu amekamilisha nusu ya muda wa mkataba wake wa miaka minne. Hivi sasa yupo na kikosi cha awali cha wachezaji 30 wa Fabio Capello wakijinoa kwa mazoezi katika kambi ya timu ya taifa ya England iliyopo Salzburg, Austria.

Wiki iliyopita mmiliki wa Villa Randy Lerner alisema klabu hiyo itafanya "kila litakalowezekana" kuhakikisha Milner haondoki.

Chelsea na Manchester United pia zimehusishwa kumuwania Milner, ingawa meneja wa United Sir Alex Ferguson ameeleza usajili msimu huu utakuwa "mgumu sana".

Villa imefanikiwa kupata nafasi ya kucheza Ligi ya Europa msimu ujao baada ya kumaliza Ligi Kuu ya England katika nafasi ya sita na isingependa kumpoteza mchezaji mwengine muhimu kwenda City baada ya msimu uliopita kumuuza Gareth Barry kwa paundi milioni 12.

City, inayomilikiwa na tajiri wa Abu Dhabi, Sheikh Mansour Bin Zayed Al Nahyan, imo mbioni kumsajili mlinzi wa kimataifa wa Ujerumani Jerome Boateng anayechezea klabu ya Hamburg kwa paundi milioni 11.

City inatarajia kusajili wachezaji wengi zaidi ili ijiimarishe kwa ajili ya kupata nafasi ya kucheza Ubingwa wa Ulaya msimu ujao baada ya msimu huu kupoteza nafasi hiyo baada ya kufungwa na Tottenham.

No comments:

Post a Comment