KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Friday, May 21, 2010

Campbell huenda akaitwa mahakamani


Waendesha mashtaka wa uhalifu wa kivita huko Hague wamesema mlimbwende Naomi Campbell anatakiwa kufika mahakamani kutoa ushahidi katika kesi ya Rais wa zamani wa Libya Charles Taylor.


Naomi Campbell
Wanasema Bi Campbell "aligaiwa almasi ambayo haikuchongwa" na Bw Taylor mwaka 1997 katika nyumba ya Nelson Mandela Afrika Kusini.

Bw Taylor anatuhumiwa kutumia "almasi zinazotoka kwenye nchi zenye migogoro ya kivita" iliyochochea uasi Sierra Leone iliyosababisha vifo vya maelfu ya watu.

Awali Bi Campbell alikataa kutoa ushahidi kwa waendesha mashtaka.

Taarifa iliyokusanywa na upande wa mashtaka kutoka mahakama maalum ya Sierra Leone imesema, " Taarifa ya Bi Campbell ni muhimu kwa vile kuna ushahidi kuwa Bi Campbell alipewa almasi ambazo hazikuchongwa na mtuhumiwa (Taylor) Septemba 1997."

Uhusiano na Mia Farrow

Bw Taylor anatuhumiwa kuuza almasi na kununua silaha kwa ajili ya waasi wa Sierra Leone wa chama cha Revolutionary United Front (RUF), waliojulikana sana kwa kukata mikono na miguu ya raia wakati wa vita vya kikatili vya wenyewe kwa wenyewe vya mwaka 1991-2001.


Charles Taylor
Aliyekuwa kiongozi wa Liberia, ambaye kesi yake imeanza tangu Januari 2008, alikana madai hayo, na kuyaita 'upuuzi mtupu.'

Amekana kuhusika na mashtaka 11 ya uhalifu wa kivita na uhalifu dhidi ya bindamu wakati wa vita vya Sierra Leone vilivyodumu kwa miaka 10.

Mapema mwezi huu, alikwepa swali kuhusu almasi wakati wa mahojiano katika kipindi cha Oprah Winfrey.

Alipoulizwa kuhusu zawadi hiyo, alisema: "Sitaki kuhusishwa katika kesi ya mtu huyu. Amefanya mambo kadhaa mabaya, na sitaki kuitia familia yangu hatarini."

Upande wa mashtaka pia wanataka muigizaji wa Marekani Mia Farrow- mgeni mwengine aliyealikwa kwenye chakula cha jioni cha Mandela- atoe ushahidi kuhusu zawadi hiyo inayoshukiwa kutolewa.

Kulingana na Bi Farrow, Bi Campbell alimwambia kuhusu zawadi hiyo asubuhi ya siku ya pili..

Bi Farrow aliiambia ABC News kuwa Bi Campbell alisema alitembelewa na wawakilishi wa Bw Taylor usiku, na walimpa almasi "kubwa" iliyokuwa haijakatwa.

Bi Farrow ameiambia ABC, " Husahau rafiki yako anapokuambia amepewa kipande kikubwa cha almasi usiku wa manane "

Ameiambia mahakama yupo tayari kutoa ushahidi atakapotakiwa.

No comments:

Post a Comment