KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Saturday, August 6, 2011

Al-Shabaab wanahama Mogadishu

Kikundi cha wapiganaji wa Kiislamu wa Somalia, al Shabaab, kinasema kuwa kimeondoka katika vituo vyake kadha ndani ya mji mkuu, Mogadishu.



Wakaazi wameiambia BBC kwamba waliona misafara ya wapiganaji ikiondoka katika mji huo.

Kuhama huko kunafuatia mapigano makali jana usiku.

Kikosi cha Umoja wa Mataifa kinachoisaidia serikali ya Somalia kimekuwa kikipigana na al Shabaab mjini Mogadishu katika siku za karibuni; ili kuweza kufikisha msaada wa chakula kwa wale walioathirika na ukame nchini Somalia.

Haijulikani kama wapiganaji hao wameondoka kabisa.

Msemaji wa serikali alielezea huo kuwa "ushindi wa dhahabu" kwa watu wa Somalia.

Lakini al Shabaab, ambayo inadhibiti sehemu kubwa ya kusini mwa nchi, ilisema wameondoka kufwatana na mikakati yao na iliahidi kufanya shambulio la kulipiza.

Baadhi ya wadadisi wanafikiri al Shabaab imepungukiwa na fedha kwa sababu wafadhili wao wa Arabuni wamewapunguzia msaada tangu al Shabaab kudhoofika kijeshi.

Wadadisi wanasema al Shabaab imewahi kuwahamisha wapiganaji wake mjini Mogadishu siku za nyuma, lakini safari hii inaonesha kuondoka kwao ni ushindi mkubwa kwa serikali.









Wengi wafa katika uvamizi Somalia






Mtoto ambaye ni mkimbizi wa ndani akila huko Mogadishu


Takriban watu watano wameuawa na wengine wengi kujeruhiwa baada ya watu wenye silaha kuvamia kambi na kuiba chakula kwenye mji mkuu wa Somalia.

Wakazi wa kambi ya Badbaado, nje ya Mogadishu, walikuwa wamepanga foleni kupata msaada wakati shambulio hilo lilipotokea.

Haikujulikana wazi ni nani alihusika na shambulio hilo japo taarifa nyingine zilisema ni askari wa serikali.

Maelfu ya Wasomali walioathirika na ukame wamewasili kwenye mji mkuu wakisaka chakula.

Katika kipindi cha miezi miwili ya nyuma peke yake takriban wakimbizi 100,000 wamefika kwenye mji mkuu huo .








Sudan 'yatishia helikopta ya UN'





Afisa mwandamizi wa umoja wa mataifa amesema, Sudan ilitishia kuidungua helikopta iliyokuwa ikijaribu kuyaondosha majeshi ya kutunza amani ya umoja wa mataifa waliojeruhiwa na mabomu ya ardhini kwenye eneo lenye mgogoro la Abyei.

Mkuu wa majeshi hayo Alain Le Roy alisema umoja huu umetumia saa tatu kujaribu kuishawishi serikali kuruhusu watu hao waondolewe kwa ndege.

Wanajeshi watatu waliojeruhiwa walifariki dunia wakati majadiliano yakiendelea, alisema.


Majeshi ya kutunza amani ya Umoja wa Mataifa


Majeshi hayo ya kutunza amani yalipelekwa mapema mwezi huu huko Abyei, eneo linalozozaniwa na Sudan na taifa jipya la Sudan Kusini.

Siku chache tu baada ya kufika Ethiopia, msafara wao uligonga mabomu hayo ya ardhini huko Mabok, kusini-mashariki mwa mji wa Abyei.

Mwanajeshi mmoja alikufa papo hapo wakati wengine watatu walifariki dunia baadae, alisema Bw Le Roy, msaidizi katibu mkuu wa majeshi ya umoja wa mataifa.

Alisema, " Hatukuruhusiwa kuondoa helikopta hiyo aina ya Medivac haraka iwezekanavyo."

"Walituzuia kuondoka kwa kututishia kuwa wataidungua helikopta."

Bw Le Roy alisema "hakuna anayeweza kusema" iwapo kuchelewa kuwaondosha wanajeshi hao kwa ndege kulichangia kwa vifo vyao.

Alisema, uchunguzi unafanywa kutokana na tukio hilo.











Ukame Kenya Waturkana 14 wafa kwa njaa




Takriban watu 14 wamekufa katika eneo la Kaskazini Mashariki katika eneo la Turkana nchini Kenya, vifo vya kwanza kutokea vinavyohusiana na njaa nchini Kenya katika eneo linalohusiana na ukame.

Mbunge wa Turkana, John Munyes, alisema vifo hivyo vimetokea katika vijiji vitatu baada ya serikali kushindwa kusafirisha chakula kwa ajili ya watu walioathiriwa na ukame.

Umoja wa Mataifa unasema zaidi ya raia wa Kenya milioni nne wanatishiwa na ukosefu wa chakula katika eneo lilikumbwa na ukame mbaya katika kipindi cha miaka 60.

Nchi nyingine zilizoathiriwa ni Somalia, Ethiopia na Djiblouti.

Mwandishi wa BBC Odiambo Joseph akiwa Turkana anasema ametembelea kijiji ambacho mamia ya watu wengi wao wakiwa wazee na dhaifu walikuwa kwenye mstri mrefu wa kugawiwa chakula.

Watu 14 waliokufa nchini Kenya walikuwa watu wazima, lakini watoto pia wana utapiamlo mkali, mwandishi wa BBC anasema.

'Watu wanahisi wametelekezwa'

Bw Munyes, ambaye ni Waziri wa Kazi katika serikali ya Muungano ya Kenya, alisema idadi ya vifo ingekuwa juu kama Shirika la Msalaba Mwekundu lisingekuwa linagawa chakula cha msaada Turkana.

"Ingekuwa ni janga," alisema.

Bw Munyes alisema vifo hivyo havikusababishwa na upungufu wa chakula bali ni ‘ukosefu wa utaratibu.’

Serikali imeshindwa kusafirisha chakula kwenye vijiji hivyo, alisema.

Mwandishi wa BBC anasema watu wengi Turkana wanahisi wametelekezwa na wametoa wito kwa jamii ya kimataifa kuiangalia kwa makini hali yao mbaya.

Umoja wa Mataifa unasema ukame umesababishwa na ukosefu wa mvua kwa miaka mingi mfululizo.

Umetangaza rasmi kuwa sehemu kadhaa za Somalia zinakabiliwa na njaa.

Karibu raia 1,300 wa Somalia wengi wao wakiwa wanawake na watoto wanaingia nchini Kenya kila siku wakitafuta chakula, Umoja wa Mataifa unasema.









Masoko ya hisa duniani yaporomoka




Bei za hisa duniani zimeshuka kwa kiasi kikubwa huku kukiwa na hofu kuhusu mwelekeo wa uchumi duniani.

Mjini New York, bei ya hisa za Dow Jones zilianguka kwa pointi mia tano kiasi kikubwa zaidi kushuhudiwa kwa karibu miaka mitatu.


Bei za hisa zimeshuka kwa kiwango kikubwa kwenye masoko duniani
Kushuka kwa bei ya hisa kumesababishwa na mgogoro wa madeni ya mataifa wanachama wa bara Ulaya huku ikiofiwa kuwa huenda Italy na Uhispania zitakabiliwa na matatizo hayo.

Pia kuna hofu kwamba huenda Marekani ikakumbwa na mdororo mwingine wa kiuchumi.

Mwandishi wa BBC mjini New York anasema kengele ya kuashiria kufungwa kwa soko la hisa mjini New York liliwapa afueni wafanyibiashara ambao siku nzima walishuhudia mauzo yakishuka kwa kasi mno.

Ikiwa chini ya miaka mitatu tangu msukosuko wa kiuchumi duniani kushuhudiwa sasa wasiwasi umezuka kuwa hali hiyo huenda inarejea.

Matukio haya bila shaka sio zawadi nzuri kwa Rais wa Marekani Barack Obama ambaye leo anasheherekea miaka 50 tangu azaliwe, na hasaa wakati uchaguzi unanukia.

Wawekezaji nchini Marekani na kote duniani wamekuwa wakiuza hisa zao na badala yake kubana pesa zao au kununua hati za dhamana za serikali ya Marekani.

Hofu kuhusu kasi ya kuimarika kwa uchumi wa marekani na pia kujikokota kwa uchumi wa nchi zingine za magharibi pia ni baadhi ya sababu za kuporomoka kwa bei za hisa.

Wadadisi wanasema kuwa hali hii huenda ikawa mbaya zaidi wakati serikali ya Marekani itakapotangaza takwimu zinazoonyesha viwango vya ukosefu wa ajira nchini humo. Dalili zinaonyesha kuwa takwimu hizo sio za kufurahisha.







Njaa ya athiri maeneo zaidi Somalia





Umoja wa Mataifa umetangaza kuwa sehemu zingine tatu nchini Somalia zinakabiliwa na baa la njaa.

Kufikia sasa kuna maeneo tano nchini humo yanayokabiliwa na tatizo hili.

Baadhi ya sehemu hizo tatu zilikuwa maarufu sana kwa uzalishaji wa vyakula.

Sehemu hizo tatu mpya zinapatikana kusini mwa Somalia na karibu na mji mkuu wa Mogadishu.


Janga la njaa Somalia


Kati ya sehemu hizo tatu, Afgoye corridor ndio ilio na idadi kubwa zaidi ya watu ikiwa na urefu wa takrbani kilomita thelathini kwenye barabara kuu inayounganisha mji wa mogadishu na ule wa Afgoye.

Wakati somalia ilipokuwa nchi thabiti, mji huu wa Afgoye ulikuwa na shughuli nyingi wak

ati wa asubuhi, malori mengi yalikuwa yakisafirisha mboga na matunda hadi kwenye soko kuu mjini Mogadishu.

Nyakati za jioni, ili kuwa jambo la kawaida kuona idadi kubwa ya mifugo ikisafirishwa, kupitia mji huo hadi soka kuu la mifugo mjini Mogadishu.

Mwaka wa 2007, eneo hili liligeuka na kuwa makao ya zaidi ya watu nusu milioni waliokimbia mapigano mjini mogadishu kati ya wanajeshi wa ethiopia na wapiganaji wa waasi.

Tangu wakati huo mji wa Afgoye umekuwa kwa kiasi kikubwa kutokana na kuongezeka kwa nyumba za mabanda na zile za kifahari.

Eneo hili la Afgoye corridor limewavutia wafanyabiashara wengi, kampuni ya simu ya mkononi na kampuni kadhaa za uchukuzi zimefungua ofisi zao katika sehemu hii.

Kutokana na kuongezeka kwa shughuli nyingi katika eneo hili, sasa limekuwa mji mkubwa ambao raia wake wanapata huduma za kimsingi kama vile shule na hospitali.

Mji wa pili uliotangazwa kuwa unakabiliwa na baa la njaa ni mji wa Balad, ulioko kilomita 40 kaskazini mwa mogadishu.

Mto shabelle umepita katikati mwa mji huo na shughuli nyingi za kilimo zinaendelea viungani mwake.

Eneo hili lilikuwa likizalisha kiasi kikubwa cha pamba ndiposa kiwanda cha kutengeneza nguo kilijengwa mjini humo.

Na mji wa tatu ni ule wa Adale, mji mdogo ulioko pwani, kaskazini mwa mogadishu.

Mji huo una sehemu nyingi zenye ufuo mzuri na wakuvutia na ni maarufu kwa shughuli za uvuvi.

Miji hii mitatu kwa sasa inathibitiwa na kundi la la wapiganaji wakiislamu la al shabaab.








Itachukua miaka 30 kuisafisha Ogoniland




Eneo la Ogoniland linaweza kuchukua miaka 30 kurejea katika hali ya kawaida baada ya mafuta kuharibu mazingira, ripoti ya UN imesema.

Ripoti hiyo ambayo imekuwa ikisubiriwa kwa muda mrefu inasema kurejesha mazingira yake ya asili kutathibisha kuwa ni eneo litakalochukua muda mrefu zaidi na kubwa zaidi kusafishwa duniani.

Ripoti hiyo imekutas kuwa athari za mazingira yanatishia afya ya jamii kwa angalau vijiji kumi katika eneo hilo.

Kampuni kubwa ya mafuta ya Shell imekiri kuhusika na matukio mawili ya kuvuja kwa mafuta yaliyoharibu mazingira katika jamii hizo mwaka 2008 na 2009.

Jamii moja ilisema itadai fidia ya mamia ya maelfu ya dola. Shell imesema italimaliza shauri hili kwa sheria za Nigeria.

Ripoti ya UN report, iliyotokna na uchunguzi wa miaka miwili, imethibitisha kuwapo kwa utata kwa sehemu kwa sababu iligharamiwa na kampuni ya Shell.

'Si ya kulaumu'

Mapema, Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa (Nep) liliwasilisha matokeo ya utafiti wake kwa Rais wa Goodluck Jonathan.

Nigeria ni mojawapo ya nchi zinazotoa mafuta kwa wingi duniani.

"Hii si tathmini iliyotayarishwa kulaumu mdau yeyote anayefanya kazi katika eneo la Ogoniland," Msemaji wa Unep Nick Nuttall amekiambia kipindi cha BBC cha Network Africa.

"Kile ambacho tuna matumaini nacho kwa makini ni kuwa hili litafunga ukurasa wa huzuni, hali tete na wakati mwingine habari za ghasia, zilizokuwa zikijirudia kwa miongo kadhaa.

"Tunatumaini kuwa hii itajenga aina fulani ya kushirikiana kati ya wadau mbalimbali katika eneo hili la dunia."

Mwandishi wa BBC Jonah Fisher mjini Lagos anasema tayari imejulikana kuwa ripoti hiyo inakuwa ikiangalia kisheria athari za miongo kadhaa za mafuta yaliyovuja kwa jamii za watu wanaoishi eneo la Ogoniland.

Alisisitiza pia kuwa kukubali kuwajibika kwa kampuni ya Shell kwa matukio ya kuvuja kwa mafuta mara mbili haihusiani na ripoti ya Unep.

Mafuta katika eneo la Ogoniland: Historia ya madhara
•1958: Mgomo wa mafuta katika Ogoniland
•1990: Vuguvugu la watu walioathirika Ogoni (Mosop)laundwa, likiongozwa na Ken Saro-Wiwa
•1993: Waogoni 300,000 waadnamana dhidi ya kutojali kwa serikali na kampuni ya Shell
•1993: Shell yajitoa Ogoniland baada ya mfanyakazi wake kupigwa
•1994: Viongozi wanne wa jumuiya ya Ogoni wauawa na kundi la vijana. viongozi wa Mosop akiwemo Ken Saro-Wiwa, wakamatwa
•1995: Bw Saro-Wiwa na wengine wanane wahukumiwa na kunyongwa; Dunia nzima yaishtumu serikali
•2003-2008: Jumuiya ya kimataifa yaelekeza macho yake kwa mgogoro wa kivita ulioanzishwa na jumuiya nyingine katika Niger Delta
•2011: Shell yakubali kuwa inawajibika katika matukio mawili ya kuvuja kwa mafuta katika eneo la Ogoniland spills
Madhara kwa viumbe

Martin Day, wakili anayewawakilisha watu wa Bodo katika eneo la Ogoniland, aliiambia BBC siku ya Jumatano kuwa eneo kubwa la limeharibiwa na mafuta akiimanisha kuwa jamii ya wafugaji haiwezi tena kuendesha maisha yake kama zamani.

"Matokeo yake, kwa hali hii hawawezi kuvua samaki," alisema. "Wameachwa, wengi wao, katika hali ya umaskini mkubwa."

Bw Day ameelezea kuwa uvujaji huo wa mafuta umekuwa miongoni mwa matukio yenye athari mbaya zaidi duniani lakini akasema umedharauliwa mpaka kampuni yake ilipotishia kuishtaki kampuni ya Shell katika mahakama nchini Uingereza.

Hili, alisema, litaweka mfano wa kisheria kwa jamii nyingine ambazo maisha yao yameathiriwa na makampuni ya magharibi.

Matatizo ya kimazingira yaliyosababishwa na biashara ya mafuta katika eneo Ogoniland kwanza yalianza kuzungumzwa na mwanaharakati Ken Saro-Wiwa, ambaye alinyongwa mwaka 1995 na serikali ya kijeshi ya Nigeria, na kuanzisha cheche za kimataifa kuhusu eneo hilo.

Kampeni hizo zimeilazimisha kampuni ya Shell kusimamisha shughuli za kuchimba mafuta kutoka eneo la Ogoniland lakini inaendelea kuendesha mabomba ya mafuta katika eneo hilo.

Ripoti iliyopita ya Unep iliwashutumu wenyeji wa eneo hilo kwa njama za wizi kuwa kwa 90% zimesababisha kuvuja kwa mafuta na kuleta athari na vuguvugu la wanaharakati wa eneo hilo.

Kabla ya ripoti hiyo harakati za Bw Saro-Wiwa kwa ajili ya uhai wa watu wa Ogoni (Mosop) zilishutumu hilo zikisema hawajashauriana na wenyeji vya kutosha.

Mwandishi wa BBC anasema huku SHELL ikiwa imegharamia ripoti hiyo, kutajwa popote kwa kampuni hiyo kubwa ya mafuta kwenye matokeo ya utafiti kutahitaji uchunguzi wa kina.










Video 'ikionyesha mateka Nigeria'


Video moja imetolewa inayodaiwa kumwonyesha raia wa Uingereza na mwenzake kutoka Italia waliotekwa mwezi Mei kwenye jimbo la Kebbi lililopo kaskazini magharibi mwa Nigeria.

Katika video hiyo, iliyotumwa kwenye shirika la habari la AFP nchini Ivory Coast, ilisema watekaji nyara hao ni kutoka kundi la al-Qaeda.

Inaonyesha mateka hao wakiwa wamezibwa macho na kupiga magoti, huku watu watatu wakiwa wamekamata silaha na kusimama nyuma yao.

Ofisi ya wizara ya mambo ya nje ya Uingereza ilisema ilikuwa ikichunguza kama video hiyo ni ya kweli na kusihi kusiwe na dhana.

Taarifa hiyo ilisema, " Tunajuta kutolewa kwa video kama hii kwa umma na tunasihi vyombo vya habari kuacha kutoa taarifa zisizothibitishwa wakati kama huu wenye utata."

Wizara ya mambo ya nje ya Italia imesihi video hiyo izuiwe na kusema ilikuwa ikifanya kazi kwa karibu na wenzake wa Uingereza na Nigeria.

Ikiwa itathibitishwa, itakuwa mara ya kwanza kwa kundi la al-Qaeda kwa upande wa Afrika kaskazini kufanya shughuli zake Nigeria, nchi maarufu barani Afrika na moja ya nchi zinazozalisha mafuta kwa wingi duniani.

Al-Qaeda inafanya shughuli zake zaidi katika eneo la jangwa la Sahara kaskazini mwa Nigeria, Niger, Mali na Algeria.

Wawili hao walikamatwa na watu wenye silaha jioni ya Mei 12 katika hoteli huko Birnin Kebbi, mji mkuu wa jimbo la Kebbi lililo mpakani na Niger.








Umoja wa mataifa wa laani Syria



Baraza la usalama la umoja wa mataifa kwa mara ya kwanza limetoa taarifa inayolaani ukiukaji wa haki za binadamu nchini Syria.

Kauli hiyo imetolewa miezi kadhaa baada ya mashauriano ya kina ambayo yalikuwa yamesababisha migawanyiko kwenye baraza hilo kuhusu matukio nchini humo.



Hata hivyo Lebanon imesitakuunga mkoto taarifa hiyo rasmi.

Taarifa hiyo haijatosheleza matakwa ya nchi za ulaya lakini hata hivyo imekuwa na uzito kando na ilivyo tarajiwa.

Hata hivyo baraza hilo limesisitiza kuwa suluhu ya mzozo unaoendelea nchini humo itapatikana kupitia machakato wa kisiasa utakaoongozwa na raia wa syria wenyewe.

Kauli hiyo imezima matumaini kuwa dola za kigeni zitaingilia kati mzozo unaoenedlea nchini humo.

Wanadiplomasia wanasema taarifa hiyo rasmi ya baraza la usalama ni onyo kwa utawala mjini Damascas.

Lakini Lebanon, hawajaunga mkono taarifa hiyo, suala ambalo halikutarajiwa ukizingatia ushawishi mkubwa wa Syria nchini humo.







Museveni aitisha kikao kujadili uchumi



Rais Yoweri Museveni ameitisha kikao cha dharura cha mawaziri kujadili jinsi ya kukabili nhali mbaya ya uchumi nchini humo.


Viongozi wa upinzani wamekuwa wakilalamikia kudorora kwa uchumi
Baraza hilo la mawaziri linakutana katika kipindi ambacho viongozi wa upinzani wamekuwa wakilalamikia kupanda kwa gharama za maisha.

Bidhaa muhimu kama vile sukari zimeanza kukosekana madukani hali ambayo inawaathiri watu wenye kipato cha chini nchini humo.

Mwandishi wa BBC mjini Kampala anasema bei ya sukari imepanda kiasi kwamba kile kiasi kilichoko aidha kinafichwa ama kuniauzwa bei kali ambayo sio ile ya kawaida.

katika maduka makubwa watu hawakubaliwi kununua zaidi ya kilo moja.

Hali hii inatishia uchumi wa taifa ambao kwa sasa kwa mujibu wa gavana wa benki kuu ya taifa kiwango cha ukuaji wa uchumi wa Uganda kitadidimia kwa asili mia 5 kutokana na kiwango kikubwa cha mfumuko wa bei za bidhaa.

Mfumuko wa bei unakaribia asili ia 20, kiwango kikubwa zaidi kwa kipindi cha maiaka 10.

Pia kiwango cha ubadilishanaji wa pesa za Uganda kwa dola kumepanda kiasi kuwa dola 1 inanunua shilling za Uganda 2,634.

Msemaji wa serikali na waziri wa habari bi Mary okurut amesema kikao hicho maalum cha mawaziri kitajadili mikakati ya kukabili hali hii ya uchumi.

Kuhusu kutoweka kwa sukari madukani, waziri Okurut amesema kuwa serikali imeomba ruhusa kutoka jumuiya ya Afrika mashariki ikubaliwe kuagizia sukari kutoka nje ya ukanda huu.

Uganda ina viwanda vitatu vinavyozalisha sukari, lakini ni kimoja tu kwa sasa kinachofanya kazi.

Viwili vilivyosalia, kimoja kimefungwa kwa sababu mitambo yake inafanyiwa ukarabati ilhali kingine kwa kuwa hakipati miwa inayotosheleza uzalishaji.









Mubarak wa Misri akana mashtaka




Aliyekuwa Rais wa Misri Hosni Mubarak amekana mashtaka ya rushwa na kuamuru kuuliwa kwa waandamanaji, siku ya mwanzo ya kesi yake iliyofanyika mjini Cairo.

Waandishi walisema, alipelekwa akiwa kwenye kitanda cha hospitali na kuwekwa ndani ya kizimba mahakamani humo, jambo lililowashtusha wengi waliokuwa nje.

Bw Mubarak mwenye umri wa miaka 83 anashtakiwa na watoto wake wawili wa kiume, ambao pia walikana mashtaka yanayowakabili, na pia aliyekuwa waziri wa mambo ya ndani Habib al-Adly na waliokuwa maafisa wengine sita.

Hukumu ya kuamuru mauaji ya waandamanaji ni adhabu ya kifo.

Takriban askari na polisi 3,000 wamezambazwa kuhakikisha kuna utulivu katika chuo cha mafunzo cha polisi ambapo kesi hiyo inasikilizwa.

Awali ilikuwa isikilizwe kwenye kituo cha mkutano cha Cairo lakini mamlaka husika zikahamisha eneo na kuunda mahakama ya muda ndani ya chuo hicho kutokana na suala la usalama.

Inakadiriwa watu 600 walitazama kesi hiyo ndani na nje ya mahakama, na mamilioni ya wengine wengi wakitazama kupitia televisheni.









Wahamiaji wa Libya wafa




Walinzi wa pwani huko Italia wamekuta miili ya watu 25 katika boti iliyokuwa imejaa wakimbizi wanaokimbia kutoka Libya.

Boti hiyo yenye mita 15 ilifunga gati katika kisiwa cha Lampedusa kusini mwa Italia iliyokuwa imebeba watu 271 waliookoka, shirika la habari la AFP liliripoti.

Miili ya watu hao 25 ilikutwa kwenye chumba chenye injini ya boti.

Maafisa walisema watu hao wameonekana kufariki dunia kutokana na kukosa hewa ya kutosha.

Maelfu ya wakimbizi kutoka Afrika magharibi wamewasili kwenye kisiwa hicho katika wiki za hivi karibuni.

Walinzi hao wa pwani waliingia katika boti hiyo siku ya Jumatatu na kugundua miili ya watu hao.

Vyombo vya habari vya Italia vimeripoti kuwa watu waliokuwa katika chumba hicho chenye injini walijaribu kutoka lakini walikwama kutokana na idadi ya watu waliokuwemo na huenda wakawa wamekabwa na harufu kali ya moshi kutoka kwenye injini.








Treni mpya ya kasi yaanza Afrika Kusini




Treni iendayo kasi barani Afrika, imeanza safari yake mpya kuelekea mji mkuu, Pretoria, kutoka Johannesburg katika jitahada za kurahisisha usafiri baina ya miji hiyo mikubwa ya Afrika Kusini.


Gautrain


Treni hiyo ijulikanayo kwa Gautrain inachukua chini ya dakika thelathini kwa safari ya umbali huo wa kilometa 54.

Kwa gari mwendo wa safari hiyo huchukua hadi saa mbili wakati watu wengi wakiwa wanatumia usafiri kwenda ama kurejea kazini.

Safari ya treni hiyo ya Gautrain kwa njia ya kueleka uwanja wa ndege ilizinduliwa wakati wa mashindano ya Kombe la Dunia mwaka 2010, ambapo maelfu ya mashabiki wa soka waliitumia kusafiria.

Lakini kwa kufika Pretoria, inaonekana itatumia zaidi na wasafiri wa kawaida nchini Afrika Kusini ili kukabiliana na foleni katika barabara yenye magari mengi nchini humo.

Mamia ya watu walimiminika katika kituo cha treni cha Rosebank mjini Johannedburg tangu mapema saa kumi na moja na nusu alfajiri kuwahi treni ya kwanza iliyoelekea Pretoria.

Kulikuwa na matatizo kidogo yalijitokeza, ikiwemo matatizo ya kiufundi katika behewa moja, lakini wahandisi wamesharekebisha tatizo hilo, kwa mujibu wa maafisa wa Gautrain.

Serikali imesema lengo lake ni kuufanya usafiri wa treni ndio uti wa mgongo wa mfumo wa usafiri wa umma, kwa mujibu wa Waziri wa Usafiri, Sbu Ndebele.

Treni hiyo ya Gautrain imegharimu randi bilioni 24 sawa na dola bilioni 3 kuijenga.

Kasi ya treni hiyo ni kilometa 160 kwa saa.

Gautrain inatarajiwa kupunguza idadi ya magari katika barabara ya N1 Ben Schoeman inayounganisha Pretoria na mji wa kibiashara wa Afrika Kusini wa Johannesburg kwa asilimia 20.










Mwandishi wa BBC awekwa kizuizini Misri






Shaimaa Khalil
Mwandishi wa BBC, Shaimaa Khalil, aliyekamatwa katika eneo la wazi la Tahrir kwenye mji mkuu wa Misri, Cairo ameachiwa huru.

Mazingira yake ya kuwekwa kizuizini siku ya Jumatatu mpaka sasa haiko wazi, lakini ilitokea baada ya wanajeshi, walioungwa mkono na polisi walipokwenda kwenye eneo walipokusanyika watu wengi kwa wiki tatu.

Walioshuhudia wameliambia shirika la habari la AFP kuwa waandamanaji walipigwa na simu zao za mkononi kuvunjwa.

Walisema, mtu yeyote aliyeonekana kupiga picha alishambuliwa.

BBC imetoa wito kwa mamlaka ya nchi hiyo kumwachia Khalil haraka iwezekanavyo.

Shirika hilo limesema katika taarifa yake, " Tuna wasiwasi sana juu ya kuwekwa kizuizini kwa Shaimaa Khalil huko Cairo. Ni mwandishi mzuri wa habari, akifanya tu kazi yake. Tunafanya kila liwezekanalo ili aachiwe."

No comments:

Post a Comment