KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Thursday, December 2, 2010

Polisi Tabora waua majambazi watano


Victor Kinambile, Tabora

POLISI mkoani Tabora, wamewaua watu watano wanaosadikiwa kuwa ni majambazi na kufanikiwa kukamata bunduki aina ya SMG, magazine tano, risasi 165 na bomu la kutupa kwa mkono.

Kwa mujibu wa Kamanda Polisi wa Mkoa wa Tabora, Liberatus Barlow, tukio hilo lilitokea juzi katika eneo la Kazima, umbali wa kilometa tano kutoka Tabora mjini, katika barabara kuu ya Tabora-Nzega.

Alisema kuuawa kwa watu hao, ni matunda ya ulinzi shirikishi unaofahamika kama Polisi Jamii.

Alisema watu hao walikuwa na mpango wa kuteka magari, lakini waligundua mpango huo na kutoa taarifa polisi.

Alisema polisi walizifanyia kazi taarifa hizo na kufanikiwa kuwakuta vijana hao, wakiwa wameweka mawe barabarani. wakisubiri malori yanayotoka mnadani kuelekea Tabora mjini.

Barlow alisema polisi walipofika katika eneo vijana waliaanza kuwarushia risasi, jambo lililowalazimisha askari, kujibu mapigo na kufanikiwa kuwaua watano ambao hata hivyo, hawajatambuliwa.

Alisema miili ya vijana hao, imehifadhiwa katika Hospitali ya mkoa wa Tabora, Kitete huku mamia ya wakazi wa mji wa Tabora, wakienda katika hospitali hiyo, kuwatambua watu hao.

Vijana waliouawa wanakadiriwa kuwa na umri wa miaka kati ya 20 hadi 25 na kwamba baadhi yao wanadhaniwa kuhusika katika matukio ya ujambazi, yaliyotokea katika Mkoa wa Tabora na mikoa ya jirani.

Kamanda alisema vijana watatu walipigwa risasi kifuani, mmoja kwenye tumbo na mwingine mgongoni.


Aliwashukuru wananchi kwa kushirikiana na polisi na kufanikiwa kuwadhibiti watu hao

No comments:

Post a Comment