KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Thursday, October 28, 2010

Rwasa aondolewa FNL


BUJUMBURA, Burundi

MGOGORO wa kisiasa unaonekana kuzidi kufukuta nchini Burundi baada ya taarifa zilizopatikana jana kueleza kwamba kiongozi wa chama cha upinzani cha FNL nchini humo, Agathon Rwasa ameondolewa katika mamlaka yake kama mkuu wa chama hicho.

Kikao hicho kilixchotangaza kumuondoa kilihudhuriwa na watu 350, wengi wao vijana na taarifa ya ufunguzi ilieleza kuwa chama cha FNL kimeamua kuisawazisha hali baada ya kupata pigo kubwa kutokana na hatua yake ya kuususia uchaguzi wabunge mwezi uliopita.

Hii ni mara ya tano wapinzani hao wa Agathon Rwasa wanajaribu kumwondoa madarakani kiongozi huyo.

Kwa mujibu wa taarifa hizo, kundi moja la chama hicho lilifanya kikao maalum ambapo Emmanuel Mibiro aliyekihama chama hicho cha FNL na kujiunga na serikali aliteuliwa kiongozi .

Mibiro ambaye awali alikuwa mshirika wa karibu wa Rwasa na ambaye chama chake kilisusia uchaguzi mkuu mwanzoni mwa mwezi uliopita kwa sasa anahudumu kama mshauri wa Rais Nkurunziza. Jacques Bigirimana ameteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa FNL.

Hata hivyo washirika wa Rwasa wamepuzilia mbali mkutano huo na kuutaja kama njama za serikali kukisambaratisha chama cha FNL.

Makamu mwenyekiti wa FNL, Alfred Bagaya alisema Agathon Rwasa ndiye kinara wa chama cha FNL na kwamba hakuna kinara mwingine anayetambuliwa na wanachama atiifu wa chama hicho.

Kundi lililomtimua Rwasa lilisema liliamua kuchukua hatua hiyo baada ya Rwasa kuamua kukimbilia mafichoni na hivyo kuhujumu shughuli za chama hasa pale alipotangaza chama hicho kususia uchaguzi mkuu Burundi, wakati yeye akiwa mgombea wa nafasi ya rais dhidi ya Nkuruzinza.

Rwasa ndiye aliyekuwa mpinzani mkuu wa Rais Nkurunziza katika uchaguzi mkuu wa mwezi Juni, ambapo hatua ya wapinzani kutangaza kususia uchaguzi huo ilimpa ushindi wa nafasi hiyo bila upinzani.

Hatua hiyo ya Rwasa kuongoza vyama vikuu vya upinzani kususia uchaguzi huo ilitokana na malalamiko yao kuhusu kuwepo kwa dosari kwenye mfumo wa uchaguzi. Kwa sasa Rwasa yupo mafichoni akihofia usalama wake

No comments:

Post a Comment