KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Thursday, October 28, 2010

Mtuhumiwa wa vurugu kampeni afia mikononi mwa polisi



Ndeninsia Lisley (RCT)

WAKATI zikiwa zimesalia siku nne kabla ya uchaguzi mkuu, imedaiwa kuwa mtu anayetuhumiwa kufanya vurugu kwenye kampeni za CCM, jimbo la Kawe amefariki dunia akiwa mikononi mwa polisi.

Kifo hicho cha Alfred Mushi, 35, kilichothibitishwa na Jeshi la Polisi kilitokea juzi wakati mtuhumiwa huyo akiwa mikononi mwa polisi na awali ilidaiwa kuwa baada ya kufanya fujo katika kampeni hizo za udiwani na ubunge za CCM, alikamatwa na kufikishwa katika kituo kidogo cha polisi cha Tegeta kabla ya mauti kumkuta.

Kamanda wa polisi wa Kanda ya Dar es Salaam, Suleimani Kova alithibitisha kutokea kwa kifo hicho akikielezea kuwa ni cha kutatanisha na kudai kuwa baada ya taarifa hiyo kutolewa kwa uongozi wa polisi wilaya ya Kawe, jalada la kifo hicho lilifunguliwa na uchunguzi kuanza mara moja ili kubaini chanzo halisi.

Alisema taarifa walizonazo ni kwamba Mushi alikuwa akijibamiza kichwa ukutani na kupiga mahabusu wengine wakati akiwa kituo kidogo cha polisi cha Kawe ambako alipelekwa na mgambo aliyemkamata na kwamba alikataa kula chakula alicholetewa na ndugu zake.

Kova aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa mtuhumiwa huyo alikumbwa na mauti hayo akiwa njiani kupelekwa Hospitali ya Mwananyamala kwa matibabu baada ya hali yake kuwa mbaya na kwamba amri ya kumpeleka hospitali ilitolewa na kamanda wa polisi na mkuu wa upelelezi wa wilaya hiyo baada ya ya hali yake kuonekana kuwa mbaya.

Kamanda Kova alisema kuwa Mushi alikamatwa Agosti 21 majira ya saa 10:00 jioni akiwa stendi ya mabasi Tegeta ambako kulikuwa na mkutano wa kampeni za kumnadi mgombea wa udiwani wa CCM.

Kwa mujibu wa Kamanda Kova, uchunguzi wa awali ulibaini kuwa Mushi alikamatwa na mgambo aliyemtaja kwa jina la Mohamed Manjolo ambaye alipewa taarifa kuwa mtu huyo alikuwa anafanya vurugu kwenye mkutano wa kampeni.

Alidai kuwa Manjolo aliwaeleza kuwa mtuhumiwa huyo alikuwa na wenzake ambao walitoroka. Alisema watu hao walikuwa wakitoa lugha za matusi na kurusha mawe kwa watu waliohudhuria mkutano huo na kwamba alionekana mlevi, hivyo walimkamata na kumfikisha kituo cha polisi.

Kova alidai kuwa Mushi alikuwa akiwapiga mahabusu wengine wakati akiwa kituoni licha ya kuonekana mlevi.

“Alikuwa akijibamiza kichwa na mwili wake kwenye ukuta ndani ya chumba cha mahabusu,” alisisitiza Kamanda Kova.

Alisema kutokana na vurugu hizo askari waliamua kumfunga pingu ili asiwadhuru wengine.

“Hata hivyo, mtuhumiwa huyo alijifungua pingu hiyo mkono mmoja, lakini mahabusu wenzake kwa kushirikiana na askari walimfunga mtuhumiwa huyo mikono,” alisema Kova.

Alisema kutokana na hali hiyo mtuhumiwa huyo hakuweza kuchukuliwa maelezo kwa mategemeo kuwa angetulia baadaye na maelezo yake kuandikwa.

Kwa mujibu wa Kamanda Kova, mahabusu wenzake walidai kuwa Mushi alikataa chakula alichopelekewa na ndugu zake.

mwelezea mtuhumiwa huyo kuwa licha ya vurugu alizokuwa akifanya ndani ya mahabusu za kujibamiza kichwa ukutani, kujifungua pingu na kumng’ata mmoja wa mahabusu kidole cha mguu wa kulia cha mwisho lakini pia alikataa hata kula chakula alicholetewa na ndugu yake

No comments:

Post a Comment