KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Monday, September 13, 2010

Njia ya kuungana upya Ujerumani imeshafunguliwa



Mkutano wa pande sita-(Ujerumani mbili) na madola manne yaliyoshinda vita vikuu vya pili vya dunia wafikia makubaliano ya kuziunganisha upya Ujerumani

Tarehe 12 Septemba mwaka 1990, mjini Moscow, mawaziri wa nje wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Ujerumani na wa Shirikisho la Jamhuri ya Ujerumani pamoja na wa madola manne yaliyoshinda vita vikuu vya pili yaani - Soviet Union, Marekani, Uingereza na Ufaransa walitia saini mkataba uliokuwa maarufu kama"mkataba kati ya wawili na wanne."Mkataba huo ulifungua njia ya kupatikana kwa muungano wa Ujerumani .

Mkataba huo ulitiwa saini baada ya kufanywa vikao vinne vya majadiliano kati ya pande mbili za Ujerumani na madola makuu manne. Majadiliano hayo yalihusika na haki ya madola hayo manne kukalia pande mbili za Ujerumani. Kuondoshwa kwa haki hiyo ilikuwa ni lazima kwa mamlaka ya Ujerumani iliyoungana. Baada ya mkataba huo kutiwa saini, waziri mkuu wa DDR alisema:

" Kilichokubaliwa ni kupunguza idadi kubwa ya vikosi. Hiyo ni hatua dhahiri inayoelekea kupunguza vikosi katika Ulaya ya Kati ambako hadi sasa kulikuwepo mkusanyiko mkubwa wa vikosi na silaha."




Waziri wa zamani wa mambo ya nchi za nje wa Shirikisho la jamhuri ya Ujerumani Hans-Dietrich Genscher

Kwa upande mwingine, mkataba huo kwa waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani ya magharibi,Hans-Dietrich Genscher, ulikuwa kipeo cha maisha yake ya kisiasa. Yeye na waziri mwenzake wa DDR Markus Meckel walifanikiwa kuondosha vikwazo vyote. Lakini jioni moja kabla ya mkataba huo kutiwa saini kulizuka matatizo ambayo hayakutazamiwa. Waziri Mkuu wa Uingereza Margaret Thatcher alikuwa na masharti zaidi kama aelezavyo Genscher:

" Alitaka kujua iwapo vikosi vya madola shirika vitaweza kufanya mazoezi yake katika DDR ya zamani au la. Lakini tatizo hilo lilitenzuliwa baada ya Soviet Union ya zamani kueleza kuwa Ujerumani yote ni mwanachama wa NATO"

Mkataba huo kati ya pande mbili za Ujerumani na washirika wanne, umetambua mipaka yote ya Ulaya, hata ule uliopo kati ya Poland na Ujerumani iliyoungana. Mpaka huo wa Oder-Neiße ulizusha mvutano uliodumu mwongo mzima katika Shirikisho la Jamhuri ya Ujerumani. Baada ya kutiwa saini, mkataba huo ulitekeleza masharti ya sera za kigeni na ulifungua njia ya kuleta muungano wa Ujerumani. Kiasi ya majuma matatu baada ya mkataba huo kutiwa saini mjini Moscow Urusi, mji wa Berlin ulikuwa na sherehe kubwa. Wajerumani walisherehekea muungano rasmi wa Ujerumani miaka 29 baada ya kujengwa ukuta wa Berlin.

No comments:

Post a Comment