KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Monday, September 27, 2010

Kura ya maamuzi Sudan kufanyika Januari


Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon na Rais wa Marekani, Barrack Obama wameliambia kongamano la Umoja wa Mataifa linaloendelea jijini New York Marekani kuwa kura ya maamuzi kuhusu uhuru wa eneo la Sudan Kusini ni sharti iandaliwe kama ilivyopangwa na kwa njia ya amani.

Viongozi hao wawili wametoa wito kwa serikali za Sudan Kaskazini na Kusini kuandaa kura hiyo, kama ilivyopangwa mwezi Januari hapo mwakani na kuheshimu matokeo yake.

Maandalizi ya kura hiyo ya maamuzi yamecheleweshwa na kiongozi wa Sudan Kusini, Salva Kirr amesema kuchelewa huko kunaweza kusababisha ghasia na machafuko.

Inaaminika kuwa raia wa Sudan Kusini watapiga kura kuunga mkono uhuru wa eneo hilo.

Wakati huo huo Muungano wa Afrika, AU, umetoa wito kwa baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, kuchelewesha mashtaka dhidi ya rais wa Sudan Omar Al Bashir kwa mwaka mmoja zaidi, ili kutohujumu maandalizi ya kura hiyo.


Mahakama ya kimataifa ya jinai ICC, imetoa kibali cha kukamatwa kwa rais Bashir, kwa shutuma za kuhusika na uhalifu wa kivita na mauaji ya halaiki katika Jimbo la Darfur magharibi mwa taifa hilo.

No comments:

Post a Comment