KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Thursday, July 1, 2010

Kifo Chasababisha Siri Ya Wake Wawili Ifichuke


Kwa miezi sita sasa maiti ya mwanaume aliyekuwa na wake wawili kwa siri nchini Bangladeshi haijazikwa kwani mke mmoja ni muumini wa Hindu anataka maiti ichomwe moto, mke mwingine ni muislamu anataka maiti izikwe kiislamu.
Mazishi ya mwanaume mmoja wa nchini Bangladesh yameshindwa kufanyika kwa miezi sita sasa kutokana na maiti yake kugombaniwa na wake zake wawili ambao walikuwa hawajuani enzi za uhai wake.

Wakati Chandan Kumar Chakrabarty mwenye umri wa miaka 42 alipouliwa kwa kuchomwa na kisu na majambazi, siri yake ya kuwa na wake wawili ilifichuka na tangu wakati huo wake zake wamekuwa wakipigania maiti yake.

Mke wake mmoja ni muislamu na alifunga naye ndoa mwaka mmoja uliopita. Mke wake huyo alisema kuwa Chakrabarty alibadili dini kuwa muislamu hivyo inabidi azikwe kwa taratibu za kiislamu.

Mke wake mwingine ndiye aliyekuwa akijulikana zaidi na alifunga naye ndoa miaka 15 iliyopita. Mwanamke huyo anasema kuwa Chakrabarty hakubadili dini yake ya Hindu hivyo inabidi maiti yake ichomwe moto igeuzwe majivu.

Mahakama nchini Bangladesh inashindwa kujua ukweli kama Chakrabarty alibadili dini kweli au la na sasa imeamua kuwahoji marafiki zake kujua ukweli wa kubadili dini kwake.

"Kama tutashindwa kupata ukweli toka kwa marafiki zake, mahakama italazimika kuamuru maiti ichunguzwe kama Chakrabarty alitahiriwa kabla ya kifo chake", alisema afisa mmoja wa mahakama.

Kutahiriwa ni suala la lazima kwa wanaume wa kiislamu lakini kwa wanaume wa Hindu si jambo la lazima.

Bangladesh ni nchi yenye waislamu wengi lakini ina idadi ndogo ya wakristo waliotokana na utawala wa Uingereza enzi za ukoloni.

No comments:

Post a Comment