KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Tuesday, June 8, 2010

Shirika la UNHCR latimuliwa Libya

Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshugulikia wakimbizi, UNHCR, limesema limelazimishwa kuondoka nchini Libya.

Msemaji wa shirika hilo ameeleza kuwa wamepata barua kutoka kwa utawala wa Libya na wameambiwa wafunge ofisi yao nchini humo.

''Utawala wa Libya haujatoa sababu zozote kusema ni kwanini wanataka tuondoke'' ameeleza msemaji huyo, Melissa Fleming.

Kila mwaka maelfu ya wahamiaji kutoka kusini mwa jangwa la Sahara hupitia nchini Libya wakielekea Ulaya.

Mabadiliko

Bi Fleming amesema hatua hiyo itakuwa na athari kubwa kutokana na sera ya nchi ya Italia kuwarejesha wahamiaji haramu nchini Libya.

Amesema shirika la UNHCR ambalo limekuwa likifanya kazi nchini Libya tangu 1991 ni muhimu sana kwa kuwa nchi hiyo haina mpango wa kuwasajili wakimbizi.

''Hatua hiyo itaacha pengo kubwa sana hasa kwa wakimbizi na watu wanaoomba hifadhi ya kisiasa'' amesema Bi Fleming.

Ameongeza kuwa takriban wakimbizi 9,000, wengi wao raia wa Palestina, Iraq,Sudan na Somalia wamesajiliwa nchini Libya.

Watu wengine 3,700 wanaotafuta hifadhi ya kisiasa ni kutoka nchi ya Eritrea.

No comments:

Post a Comment