KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Friday, May 28, 2010

Mourinho sasa ni meneja wa Real Madrid

Klabu ya Real Madrid ya Uhispania imetangaza kwamba itamjulisha Jose Mourinho rasmi kwa mashabiki wao, Jumatatu ijayo.
Klabu kilitoa taarifa kuthibitisha hayo.

Marais wa vilabu vya Inter Milan ya Italia, na Real Madrid, walikutana Ijumaa mjini Milan, Italia, kutatua masuala yote, hasa ya kifedha, kuhusiana na Jose Mourinho kuhama kutoka Inter, na kuelekea Uhispania.

Real Madrid wameshawahi kunyakua ubingwa wa Ulaya mara tisa.

Jose Mourinho anaondoka Inter baada ya msimu uliokuwa wa fanaka mno, kupata ushindi katika mashindano matatu muhimu Italia, ikiwa ni pamoja na kuwa klabu bingwa barani Ulaya.

Hata hivyo klabu ya Inter haikutoa maelezo kamili katika taarifa hiyo, kuhusu mapatano hayo kati ya rais wa klabu Massimo Moratti na mwenzake wa Real, Florentino Perez.

Lakini vyombo vya habari nchini Uhispania vimekuwa vikielezea kwamba Inter watapata euro milioni nane, ambazo ni sawa na dola milioni 9.80.

Mourinho aliiongoza Inter kupata vikombe vitatu muhimu, na alimalizia kwa ushindi katika fainali ya klabu bingwa Ulaya, dhidi ya Bayern Munich ya Ujerumani katika uwanja wa Bernabeu, mjini Madrid.

No comments:

Post a Comment