KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Saturday, May 29, 2010

Mataifa 200 kupunguza silaha za nuclear

Mataifa takriban 200, wanachama wa mkataba uliotia sahihi ya upunguzaji wa silaha za Nuclear (npt) yameafiki mpango wa jitihada za kulifanya eneo la Mashariki ya kati lisilo kuwa na silaha hizo.
Kwenye mkutano uliofanywa kwenye makao makuu ya Umoja wa mataifa mjini New York wajumbe waliitisha mkutano mnamo mwaka 2012 utakaohudhuriwa na mataifa ya mashariki ya kati-ikiwemo Iran kuunda eneo huru ya bila silaha za nuclear.

Waraka huo ulioafikiwa kwa sauti moja uliitaka Israel nayo isahihishe mkataba wa kupinga nuclear.

Lakini Rais Barack Obama aliyekubali mpango huo amepinga kuitenga Israel kwa kusema kuwa hilo linaweza kuathiri juhudi za kuishawishi nchi hiyo isihudhurie mazungumzo ya mwaka 2012.

Baadaye Afisa wa Israel aliutaja waraka huo kama uzandiki. Alisema kuwa, Israel imetajwa, il hali waraka haukutaja nchi kama India,Pakistan na Korea ya kaskazini ambazo zina zana za nuclear, pamoja na Iran ambayo inajitahidi kujenga silaha kama hizo, afisa wa ngazi ya juu aliliambia shirika la habari la Ufaransa(AFP)

Waraka huo wenye kurasa 28 ulisahihishwa na nchi wanachama 189 kufuatia mazungumzo nyeti mnamo siku ya mwisho wa mazungumzo ya mwezi mzima yaliyokusudia kuimarisha fungamano la mkataba unaotaka kupunguza matumizi ya nuclear, kama nguzo muhimu katika juhudi za kimataifa za kuondoa silaha.

Waraka huo unamtaka katibu mkuu wa Umoja wa mataifa kuandaa mkutano wa mataifa ya mashariki ya kati mnamo mwaka 2012 ili kuafikiana juu ya kuunda eneo lisilo kuwa na silaha za nuclear pamoja na silaha nyingine za maangamizi.

Rais wa mkutano huo, Libran Cabactulan kutoka Ufilipino amesema kuwa dunia yote inatuangalia sisi wakati waraka huo unaidhinishwa.

Mjumbe wa Misri, Maged Abedelaziz, akizungumza kwa niaba ya Vuguvugu la mataifa yasiyofungamana na siasa za upande wowote, alifurahia uwamuzi na kusema ni hatua muhimu katika kufikia malengo ya mkataba.

Wajumbe walijadili mapendekezo hadi usiku wa manane kabla ya kuyarejelea tena hapo jana asubuhi.

Mojapo ya hoja kuu ziliihusu Israel ambayo si mwanachama wa fungamano hili la mkataba unaodhamiria kupunguza silaha za nuclear, inaaminika kuwa na silaha za nuclear ingawaje haijawahi kukubali kuwa nazo.

Ilikuwa kazi ngumu kwa wajumbe wa nchi za Kiarabu na marafiki wa Israili ili kuweza kuafikiana juu ya maneno yanayostahili kutumika kuandika mkataba huu. Waandishi wa habari wanasema kuwa mataifa ya kiarabu yanataka kuishinikiza Israili isalimishe zana zake za nuclear.


Iran nayo ilitaka mataifa matano yanayomiliki silaha za nuclear yakubaliane juu ya mpango wa tareh ya kusalimisha silaha zake.

Katika waraka kamili ulioafikiwa hakuna mda uliowekwa lakini mataifa hayo lazima yaharakishe hatua za kufikia lengo hili la kupunguza silaha za nuclear na wakutane tena mnamo mwaka 2014.

No comments:

Post a Comment