KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Sunday, May 16, 2010

Hofu ya mafuriko nchini Kenya

Serikali ya Kenya imesema imeanza kuhamisha watu wanaoishi karibu na Mto Tana na kuonya kuwa huenda mabwawa matatu yakafurika katika muda wa siku chache zijazo.

Mkuu wa shughuli za dharura nchini Kenya, Kanali Vincent Anami, amesema bwawa la Masinga limesalia kimo cha mita moja tu kabla ya kuanza kufurika.

Kuna hofu kuwa hali hiyo itasababisha mafuriko makubwa sana katika maeneo ya kaskazini-mashariki na mashariki mwa nchi hiyo.

Shirika la msalaba mwekundu linasema watu 81 wamekufa na wengine 130,000 wameathiriwa na mafuriko hayo na pia maporomoko ya ardhi na pia limeonya kuwa huenda kukatokea magonjwa ya kuambiza.



Msemaji wa shirika hilo, Nelly Muluka, amesema idadi ya watu walioathirika na mafuriko hayo inatarajiwa kuongezeka.

''Mvua inayoendelea kunyesha imesababisha hali kuwa mbaya zaidi hasa kwa watu walioathiriwa na baa la njaa mwaka jana na tumezindua ombi la dola millioni 6 ili kuwasaidia," alisema Bi Muluka.

Serikali imewashauri watu wanaoishi karibu na mito kuondoka ili kuepuka mafuriko hayo.

Mvua kubwa inayoendelea kunyesha katika eneo la Afrika Mashariki imesababisha mafuriko na maporomoko ya ardhi siyo tu nchini Kenya lakini pia Tanzania na Uganda.

No comments:

Post a Comment