KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Friday, May 7, 2010

Hakuna mshindi wa jumla uchaguzi Uingereza


Chama cha Conservative kinaongoza kwa idadi ya viti huku matokeo ya uchaguzi mkuu wa Uingereza yakitarajiwa kukamilika.

Mpaka alfajiri ya Ijumaa, chama hicho kilikuwa kimeshapata viti 281 kati ya 650 wakati Labour kinachoongozwa na Waziri Mkuu wa sasa Gordon Brown kilikuwa kimekusanya viti 227 na Liberal Democrats kilipata 48.

Matokeo zaidi yataendelea kupatikana kabla ya picha halisi ya waingereza walivyopiga kupatikana.

Hata hivyo, hakuna chama kitakachopata viti vingi kiasi cha kutosha kuunda serikali mpya bila kushirikiana na vyama vingine. Idadi ya viti vinavyotakiwa kukiwezesha chama kupata ushindi wa jumla ni 326.

Serikali mpya

Hali hiyo inaweza kumruhusu Waziri Mkuu Gordon Brown kuendelea kuwa madarakani kwa mujibu wa sheria ya Uingereza, ingawa wachambuzi wengi wa maswala ya kisiasa wanadhani David Cameron ana nafasi kubwa ya kuwa Waziri Mkuu mpya.

Idadi ya wapiga kura imeelezewa kuwa ni kubwa kuliko ilivyokuwa kwenye uchaguzi uliopita. Kumekuwa na taarifa za idadi kubwa ya wapiga kura kurejeshwa nyumbani baada ya muda wa mwisho kumalizika saa nne usiku katika miji mbali mbali kama London, Birmingham na Leeds.

No comments:

Post a Comment