KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Thursday, October 28, 2010

Tsunami yaua watu wengi Indonesia



Zaidi ya watu 100 wameuawa na wengine wengi hawajulikani walipo kufwatia tsunami iliyosababishwa na tetemeko la ardhi katika pwani ya Sumatra nchini Indonesia.

Maafisa wanaoshugulika na misaada pia wanajaribu kukabiliana na athari za mlipuko wa volkeno katika Mlima Merapi Katikati mwa Java.




Nyumba kadhaa ziliharibiwa na mawimbi ya bahari karibu na visiwa vya Mentawai.

Maji yaliyofurika yaliharibu kabisa vijiji kumi kwenye visiwa hivyo, afisa mmoja anayeshughulika na uokoaji aliambia shirika la habari la AFP.






Baadhi ya watu walioachwa bila makao
Hali mbaya ya hewa na uharibifu imechelewesha juhudi za kufikia maeneo yaliyoathirika.




Hendri Dori Satoko,mjumbe katika visiwa vya Mentawai,aliambia kituo cha televisheni cha Metro: "takwimu zetu za hivi punde zinaonyesha kuwa watu 108 wameuawa na wengine 502 hawajulikani walipo."

Alisema baadhi ya wale ambapo hawajulikani walipo huenda walikimbilia maeneo salama ya juu na wanaogopa kurudi nyumbani kwao.

Maafisa wa wizara ya afya wanasema miili 113 imepatikana katika eneo hilo kufikia sasa,shirika la habari la Associated Press limeripoti.

Wakati huohuo maafisa wanasema zaidi ya watu elfu kumi na tatu wamehamishwa kutoka maeneo ya karibu na Mlima Merapi na kupelekwa katika kambi tangu mlipuko wa volkeno kutokea.

Lakini hali imeelezewa kuwa ngumu kutokana na idadi kubwa ya watu wanaotaka kuhama na kutafuta hifadhi katika maeneo salama.

Wakaazi wengi wa vijiji vilivyo karibu walipuuza onyo lililotolewa hapo awali na maafisa na hawakuwa tayari kuondoka na kuacha makao na mashamba yao

No comments:

Post a Comment