KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Thursday, September 2, 2010

N'dour wa Senegal azindua televisheni



Mwanamuziki wa miondoko ya Pop kutoka Senegal Youssou N'dour amezindua rasmi kituo chake cha televisheni baada ya kusumbuana na serikali ya nchi hiyo kwa miaka miwili.

Mwanamuziki huyo tayari anamiliki kampuni yake binafsi inayoshughulikia vyombo vya habari huko Dakar, inayokusudia kuipinga serikali ya nchi hiyo.

Waandishi wanasema, kituo hicho kipya, TFM, kitaonyesha masuala ya kiutamaduni, baada ya serikali kumnyima leseni ya kuonyesha mambo mengine tofauti.

Bw N'dour kwa sasa ana matumaini ya kuzifikia nchi jirani.


Youssou N'dour


Mwandishi wa BBC wa Afrika magharibi aliyopo Dakar Thomas Fessy alisema mwanamuziki huyo ana matumaini ya kampuni yake kuwa shirika kuu la habari eneo hilo la magharibi ya Afrika.

Kituo chake cha redio, kilichozinduliwa miaka saba iliyopita, kina mafanikio makubwa na ina wasikilizaji wengi katika mji mkuu wa Dakar.

Mhariri wa redio hiyo Allassane Samba Diop, ambaye atafanya kipindi kimoja katika televisheni hiyo ya TFM (Television Future Medias), aliiambia BBC kwamba "utamaduni" inawanyima nafasi ya kufanya vipindi vingi.

Alisema bado itakiruhusu kituo hicho kuandaa masuala ya kijamii, kisiasa na kiuchumi. TFM ni televisheni ya tano ya kibinafsi nchini humo.

Youssou N'dour aliimba na kutoa hotuba kuadhimisha uzinduzi huo.

"Katika ulimwengu ambao watu zaidi wanaathiriwa na nguvu ya picha na kasi ya habari, nina furaha kusema kwamba serikali ya Senegal imechukua uamuzi sahihi tarehe 11 Mei 2010, kuruhusu TFM kufanya matangazo."

Ushawishi wa kisiasa?
Mashabiki walifurahia uzinduzi huo.

Mshabiki mmoja Saliou Diouf, "Tunaomba Mungu aibariki televisheni yake.....Tunamtakia kila la kheri tukiwa na matumaini, huku tukimshukuru Mungu, atafanikiwa kwa yale aliyoyakusudia na televisheni hii."

Mtafaruku wa leseni ulianza rasmi kutokana na namna televisheni hiyo itakavyodhaminiwa.

Rais wa Senegal Abdoulaye Wade awali alisema leseni ya kurusha matangazo imekataliwa ili kuzuia "watu wa kigeni" kutoa ushawishi wa sera zao.

Mwandishi wa BBC mjini Dakar Tidiane Sy alisema, Bw N'dour alitumia umaarufu wake kama mwanamuziki, kuwakusanya maelfu ya wafuasi kumwuunga mkono na hatimaye akafikia muafaka na serikali.

Mwandishi wetu aliongeza, Bw N'dour alisema hivi karibuni kwamba hatowania urais, lakini atamwuunga mkono anayegombea urais katika uchaguzi ujao, unaotarajiwa kufanyika mwaka 2012.

No comments:

Post a Comment