KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Tuesday, August 24, 2010

Walaani amri ya mahakama: Afrika Kusini




Vyama vya wafanyakazi vya Afrika Kusini vimelaani amri ya mahakama iliyofuatia maombi ya serikali kupiga marufuku wafanyakazi wa umma kuendelea na mgomo wa kitaifa.
Msemaji wa shirikisho la vyama vya wafanyakazi kutoka Cosatu ameiambia BBC kuwa hatua hiyo ina lengo la 'kuwatisha' wafanyakazi wanaogoma.

Siku ya Jumamosi, serikali ilituma wanajeshi ambao ni madaktari kuhudumia hospitali 32.

Zaidi ya wafanyakazi milioni moja wapo katika mgomo tangu Alhamisi, wakitaka malipo zaidi.
Afrika Kusini

Polisi walitumia risasi kupambana na waliogoma

Serikali ilipata amri ya mahakama dhidi ya vyama vya wafanyakazi mapema siku ya Jumamosi. Serikali ilisema hatua hiy ilihitajika ili hospitali ziweze kutoa huduma na magereza kuwa na wafanyakazi.

Amri hiyo ya mahakama pia inakataza wauguzi na walimu kuwatisha wenzao ambao wamegoma kushiriki katika mgomo huo.

Mhariri wa masuala ya Afrika wa BBC Martin Plaut anasema mgomo huo unaonekana kushika kasi, huku vyama viwili zaidi vya walimu vikijiandaa kuungana na mgomo huo, na kuna dalili ndogo za kuonesha mgomo huo utapatiwa ufumbuzi kirahisi.
Vyama vya wafanyakazi, ambavyo vinawakilisha wafanyakazi milioni moja wa umma, wanatuhumu polisi kwa kuwatisha wanachama wao.

Shule zimefungwa, hospitali na barabara zimewekewa vikwazo.

Serikali imesema itatoa ongezeko la asilimia saba. Vyama vya wafanyakazi vinavyoshirikiana na Cosatu vimesema vinataka ongezeko la asilimia 8.6.

Serikali imesema haina uwezo wa kutoa ongezeko la mshahara ambalo thamani yake ni mara mbili ya kiwango cha mfumuko wa bei.

Licha ya amri hiyo ya mahakama, vyama vya wafanyakazi vimesema havitawaambia wanachama wake kurejea kazini.

Siku ya Ijumaa, waziri wa afya Aaron Motsoaledi alisema wafanyakazi wa hospitali waliovuruga huduma muhimu za kiafya na kulazimisha wafanyakazi wenzao kushiriki katika mgomo, vitendo vyao vinafanana na kufanya mauaji.

Rais Jacob Zuma ametetea msimamo wa vyama vya wafanyakazi, lakini pia amewataka kuacha ghasia na vitisho.

No comments:

Post a Comment