KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Thursday, May 6, 2010

Msaada kwa Ugiriki utawanufaisha Wajerumani pia


Baada ya nchi za kanda ya sarafu ya Euro kuamua kuisaidia Ugiriki, sasa serikali ya Ujerumani ndio inapigia debe kupata idhini ya bunge lake kuhusu ile sehemu itakayochangwa na Ujerumani katika msaada huo wa fedha.

Serikali mjini Berlin haina wakati wa kupoteza, kwani mpango huo wa kuisaidia Ugiriki unapaswa kuidhinishwa juma hili. Katika hatua ya kwanza, baraza la mawaziri limeshaunga mkono msaada huo wa euro bilioni 110 utakaotolewa katika kipindi cha miaka mitatu ijayo.

Shirika la Fedha la Kimataifa IMF litatoa euro bilioni 30 na nchi za kanda inayotumia sarafu ya Euro zitachanga euro bilioni 80 ameeleza Kansela wa Ujerumani Angela Merkel. Sehemu ya Ujerumani ni asilimia 28 - hiyo humaanisha katika kipindi cha miaka mitatu ijayo ni kama euro bilioni 22.4. Katika mwaka wa kwanza itahitaji kutoa euro bilioni 8.4 na zingine bilioni 14 katika mwaka 2011 na 2012.Akaongezea:

"Kulingana na ukubwa wake,Ujerumani ndio inayobeba sehemu kubwa ya mzigo huo.Kuambatana na mpango huo,mikopo itatolewa na taasisi ya mikopo ya ujenzi mpya na itadhaminiwa kwa bajeti ya serikali."

Merkel amesisitiza kuwa hatimae msaada huo utawanufaisha Wajerumani vile vile. Hata Waziri wa Fedha Wolfgang Schäuble ameunga mkono kauli hiyo na kuongezea kwamba haikuwa rahisi kwa serikali ya Ujerumani kukubali kuipa Ugiriki mkopo wa mabilioni. Lakini hapo kilicho muhimu ni kuimarisha sarafu ya Ulaya na hivyo kuhifadhi muungano wa Ulaya. Schäuble amesema:Bildunterschrift: Großansicht des Bildes mit der Bildunterschrift: Waziri wa Fedha wa Ujerumani, Wolfgang Schäuble.
"Huo sio ubadhirifu wala kukubali hasara za uwekezaji usiowajibika, bali ni kutambua jukumu letu kwa maslahi ya siku zijazo.

Lakini sera za serikali zimekosolewa vikali na upande wa upinzani. Kiongozi wa chama cha SPD, Sigmar Gabriel, amesema kuwa Merkel alijaribu kutumia ujanja ili asitaje kiwango cha msaada, kabla ya uchaguzi wa jimbo la North Rhine Westphalia. Kusitasita kwake, ndio uliowapa walunguzi fursa ya kupandisha riba ya mikopo.Kwa maoni yake, mbinu hizo za kuyumbayumba zimesababisha hasara kubwa kwa walipakodi wa Ujerumani na Ulaya. Merkel alibadili msimamo wake baada ya kushinikizwa na IMF na Umoja wa Ulaya.

Chama cha SPD bado hakijakubaliana msimamo wa kuchukuliwa bungeni. Mwenyekiti wa wabunge wa SPD,Frank-Walter Steinmeier anataka sekta ya mabenki binafsi, ichangie kuisaidia Ugiriki. Hata chama cha Kijani kinadai kuwa mabenki pia yabebebshwe jukumu hilo. Kiongozi wa wabunge wa chama cha Kijani Jürgen Trittin amesema, ni matumaini yao kuwa katika siku zijazo kutachukuliwa hatua zitakazopunguza hatari ya mzozo kama huo kutokea mara nyingine tena.

Mswada wa sheria ya kuidhinisha mpango wa kuisaidia Ugiriki, unapaswa kupitishwa hadi ifikapo Ijumaa, ili uweze kutiwa saini na Rais wa Ujerumani Horst Köhler kabla ya mwisho wa juma na hivyo kuweza kufanya kazi.


Mwandishi:Marx,Bettina/ZPR/P.Martin

Mhariri: Aboubakary,Liongo

No comments:

Post a Comment