KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Saturday, February 20, 2010

UN yaikosoa Marekani kuhusu Somalia




Umoja wa mataifa unasema masharti yaliyowekwa na Marekani ya kutoa msaada kwa Somalia yanasababishia raia mateso makubwa.
Mratibu wa misaada ya kibinadamu nchini Somalia Mark Bowden ameilaumu Marekani kwa kuligeuza swala la msaada kuwa la kisiasa katika juhudi zake za kuhakikisha misaada haiwafikii wanamgambo wa Kiislamu wanaodhibiti eneo kubwa la nchi.

Umoja wa mataifa unakadiria kwamba katika eneo moja la Somalia , asilimia 70 ya watu wanahitaji msaada wa chakula ili kuendelea kuishi.

Lakini Bw Bowden amesema mashirika ya kimisaada hayawezi kutimiza masharti yaliyotolewa na Marekani ambayo ndio mfadhili mkuu wa misaada nchini Somalia.

Yar'Adua kusalia kuwa rais wa Nigeria




Baraza la mawaziri nchini Nigeria limepinga mswaada uliolenga kumondolea mamlaka rais Umaru Yar'Adua kwa msingi kuwa anaugua kiasi cha kutoweza kuongoza nchi tena.
Waziri wa habari Dora Akunyili amesema baraza limeamua badala yake, kutuma tena ujumbe mwingine nchini Saudi Arabia kumjulia hali rais Yar'Adua ingawa hakusema ni lini ujumbe huo utaondoka.

Rais Yar'Adua anaendelea kupokea matibabu nchini Saudi Arabia kwa zaidi ya miezi mitatu sasa.

Thuluthi mbili ya wabunge wa Nigeria ndio wanaweza kupitisha mswaada kama huo . Wiki iliopita makamu wa rais Goodluck Jonathan, alichukua wadhifa wa kaimu rais kufuatia agizo la bunge.

ARV'S zazuia maambukizi ya HIV


Utafiti mpya umeonyesha kuwa dawa zinazotumika kutibu maradhii tegemezi kwa wagonjwa wa ukimwi (ARVS) zinaweza kuzuia maambukizi ya virusi vya HIV.
Utafiti uliofanywa miongoni mwa wanandoa elfu tatu mia tano wanaogua virusi hivyo barani afrika , ulionyesha kuwa uwezekano wa wagonjwa waliotumia sana dawa za ARV,'s kuwaambukiza wenzao, ni wa chini mno.

Kwa kipindi cha miaka mitatu, zaidi ya visa mia moja vya maambukizi mapya ya HIV viliripotiwa miongozi mwa waliokuwa wanafanyiwa utafiti huo. Lakini ni mtu mmoja tu aliyekuwa anatumia dawa hizo ndiye alieambukizwa.

Waliofanya utafiti huo, wanasema huenda mtu huyo aliambukizwa kutokana mabadiliko mwilini mwake yaliosababishwa na dawa hizo.

Ulaya yaishinikiza Israel




Shinikizo zimeendelea kuwepo dhidi ya Israel za kuitaka itoe maelezo kuhusu kutumiwa kwa pasipoti za ulaya na watu wanaoshukiwa kumwuua mwanamgambo mmoja wa Palestina nchini Dubai mwezi uliopita.
Waziri wa mambo ya nje wa Uingereza David Miliband amesema serikali ya Uingereza inatarajia Israel kutoa ushirikiano katika uchunguzi wa kesi hiyo, baada ya maafisa wa serikali ya Uingereza kukutana na balozi wa Israel kwenye ofisi ya mambo ya nje kuelezea wasi wasi wao.

Ufaransa na Ireland pia zimechukua hatua sawa na hiyo ya Uingereza.

Bwana Miliband amesema hangependa nchi zingine ulimwenguni kupoteza imani na paspoti za Uingereza.

Amesema pasipoti zilizotumika katika tukio hili hazikuwa na teknolojia mpya ya sasa inayotumia chipu ya kuhakikisha kwamba hazitumiki vibaya.

Annan awaasa Kibaki na Raila




Kundi la viongozi mashuhuri wa Muungano wa Afrika limeelezea wasiwasi wake kuhusu mzozo wa kisiasa unaoendelea nchini Kenya, na kusema kuwa huenda ukaathiri utekelezwaji wa mkataba wa kitaifa wa serikali ya muungano.
Katika taarifa yao, kundi hilo linalo-ongozwa na aliyekuwa katibu mkuu wa umoja wa mataifa na mpatanishi mkuu katika mzozo nchini Kenya, Kofi Annan, limewataka rais Mwai Kibaki na waziri mkuu Raila Odinga wafanye mashauriano ili kuutatua mzozo huo.

Mvutano wa hivi punde kati ya Rais Kibaki na waziri mkuu Raila Odinga ulianza siku ya jumaapili, wakati Bw Kibaki alipobatilisha uamuzi wa awali wa Bw Odinga wa kuwasimamisha kazi mawaziri wawili waliohusishwa na kashfa za ufisadi.

Kufuatia hatua hiyo, Bw Odinga alitoa wito kwa Bw Annan kuja kuutatua mzozo huo.

Lakini taarifa ya jopo hilo la watu mashuhuri imemnukuu Bw Annan akitoa wito kwa waakilishi wa pande mbili walioshiriki katika kubuni mwafaka wa serikali ya muungano kutilia mkazo kutekeleza ajenda za mwafaka huo.

Jopo hilo limeelezea wasi wasi kwamba huenda mzozo uliopo ukatatiza juhudi za kupambana na ufisadi katika serikali ya Kenya.

Awali Rais Kibaki alisema hakuna mzozo wowote katika serikali ya Kenya.

AU, ECOWAS zapinga mapinduzi Niger




Muungano wa kiuchumi wa nchi za Afrika magharibi ECOWAS umetuma ujumbe kwenda Niamey, mji mkuu wa Niger, kuelezea pingamizi za muungano huo kuhusu mapinduzi ya kijeshi yaliyomwondoa madarakani Rais Mamadou Tandja.
Msemaji wa ECOWAS amesema muungano huo unazingatia sera za kutokubali madaraka katika nchi yoyote kutwaliwa pasipo kufuata katiba ya nchi.

Umoja wa Afrika, AU, pia kupitia mwenyekiti wa tume ya AU Jean Ping umelaani mapinduzi hayo ya Niger.

Viongozi wa kijeshi walioipindua serikali ya Bw Tandja wameahidi kuigeuza nchi hiyo kuwa mfano bora wa nchi inayozingatia demokrasia na utawala bora.

Afisa mmoja wa ngazi za juu Kanali Salou Djibo ametangazwa kuwa kiongozi wa serikali ya kijeshi.

China yaghadhabishwa na Marekani




Serikali ya china imeelezea kughadhabishwa na mkutano uliofanyika kati ya kiongozi wa kidini wa Tibet Dalai Lama na rais Barack Obama.
Saa chache tu baada ya mkutano huo, china, ambayo imekuwa ikisanifu mienendo ya kiongozi huyo wa kidini, ilisema kuwa mkutano huo ulikiuka sheria za kimataifa na sera za kigeni za marekani.

Imesema pia kuwa Marekani lazima ikome kuwaunga mkono maadui wake.

Baada ya mkutano huo msemaji wa Rais Obama ameelezea kuwa Obama alipongeza juhudi za Dalai Lama za kupinga mapinduzi kwa kutumia nguvu na badala yake kuegemea mashauriano na china.

Wamisri wakatazwa kumpokea ElBaradei


Vikosi vya kiusalama nchini Misri vimewazuia wafuasi wa upinzani kukusanyika katika uwanja wa ndege kumkaribisha aliyekuwa mkuu wa shirika la kimataifa la nguvu za Atomiki Mohammed ElBaradei, ambaye anakusudia kugombea Urais.
Wanaharakati wa upinzani wamekuwa wakitoa wito ElBaradei apewe makaribisho yanayostahiki shujaa, lakini mikutano ya hadhara sio halali nchini Misri na inaweza kuvunjwa na Polisi.

Bw ElBaradei alijenga sifa kubwa kimataifa alipokuwa mkuu wa shirika la IAEA , na alishinda tuzo ya Nobel mwaka 2005.

Anaonekana mwenye uwezo mkubwa wa kutoa upinzani kwa Rais Hosni Mubarak kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka ujao.

Tiger Woods amuangukia mkewe Elin


Mcheza gofu mashuhuri duniani Tiger Woods katika mkutano wa waandishi wa habari amemuomba radhi rasmi mkewe kwa kumuendea kinyume.
Mcheza gofu huyo anayeshikilia nafasi ya kwanza kwa ubora duniani, alikuwa akizungumza hadharani kwa mara ya kwanza tangu kashfa iliyokuwa imegubika maisha yake ya faragha kuibuka mwezi wa Novemba mwaka jana.

Woods Mmarekani mwenye umri wa miaka 34 alikuwa akihutubia kundi dogo la marafiki, wacheza gofu wenzake na jamaa wa karibu mjini Florida.

Mcheza gofu huyo aliyewahi kushinda mataji makubwa mara 14 alisema hakuwa mwaminifu, alikuwa na uhusiano na wanawake wengine na alitembea nje ya ndoa. Alikiri kitendo hicho ni cha fedheha na hakikubaliki.

Aliendelea kukiri, kwa vitendo vyake amemuumiza mkewe, wanawe, mama yake, familia ya mkewe, mfuko wake na watoto wote duniani waliokuwa wakimpenda.

Woods alisema kuna uwezekano wa kurejea kucheza tena gofu mwaka huu, lakini akasema bado hajapanga tarehe na akaongeza atarejea tena kupata nasaha na ushari siku ya Jumamosi.

Alisema ni vigumu kukiri lakini anahitaji msaada.

Tiger Woods alifafanua kwamba kwa siku 45 tangu mwishoni mwa mwezi wa Desemba hadi mapema mwa mwezi wa Februari, alikuwa akipatia matibabu ya kitaalamu ya kumuweka sawa na dhoruba hiyo ya maisha aliyokumbana nayo.

Alisema anasafari ndefu katika hilo lakini amekamilisha hatua ya awali ya safari hiyo kwa njia sahihi.

Terry ang'olewa unahodha England


Terry ang'olewa unahodha England

John Terry amevuliwa unahodha wa timu ya taifa ya England kutokana na madai ya kuwa na uhusiano wa kimapenzi na mpenzi wa mchezaji mwenzake.

Terry, mwenye umri wa mika 29, kabla ya uamuzi huo alifanya mazungumzo na kocha Fabio Capello wa England katika uwanja wa Wembley siku ya Ijumaa.

"Baada ya kutafakari kwa muda mrefu, nimeamua kwamba litakuwa jambo jema kwangu kumvua John Terry unahodha," alieleza Capello katika taarifa.

Terry mlinzi wa Chelsea ambaye amerithiwa wadhifa huo na mlinzi mwenzake Rio Ferdinand, alisema anaheshimu uamuzi wa Capello kumng'oa yeye.

Friday, February 12, 2010

Blatter atetea waandalizi wa kombe la dunia




Rais wa shirikisho la soka ulimwenguni, FIFA, Sepp Blatter, amewashutumu wanaokosoa kuandaliwa kwa kombe la dunia mwaka huu Afrika Kusini.
Rais wa klabu ya Bayern Munich ya Ujerumani, Uli Hoeness, amenukuliwa akisema FIFA, ilifanya kosa kubwa kuipa Afrika Kusini nafasi ya kuandaa mashindano hayo. Lakini Blatter amesema matamshi hayo ni ya kudunisha bara la Afrika na hayana msingi wowote.

Kocha wa klabu ya Hull City, Phil Brown amesema kushambuliwa kwa timu ya Taifa ya Togo, wakati wa mashindano ya kombe la mataifa bingwa barani Afrika, nchini Angola, kunazua hali ya wasi wasi kwa timu zitakazoshiriki katika fainali ya kombe la dunia nchini Afrika Kusini.

Watu wawili waliuwawa, waasi waliposhambulia basi la timu hiyo katika eneo la Cabinda. Lakini Blatter amesema tukio hilo lililotokea nchini Angola halina uhusiano wowote na maandalizi ya kombe la dunia.

Viongozi wa Rwanda watishia wakosoaji




Shirika la kutetea haki za binadamu la Human Rights Watch limesema, serikali ya Rwanda inawashambulia na kuwatishia wakosoaji wa uongozi wa nchi hiyo inayoelekea kwenye uchaguzi wa Rais mwezi Agosti.
Shirika hilo limesema viongozi wanawalenga upinzani kwa madai kuwa walishiriki katika mauaji ya kimbari ya mwaka 1994.

Msaidizi wa kiongozi wa upinzani amefungwa kwa uhalifu wa mauaji hayo, lakini amedai kuwepo nje ya nchi wakati huo.

Rais Paul Kagame amesema anaheshimu haki za watu lakini hatomvumilia yeyote anayevuruga amani na utulivu.

Hata hivyo, Human Rights Watch limesema vitisho kwa upinzani inavuruga demokrasia.

Goodluck atikisa baraza la mawaziri Nigeria




Katika siku yake ya kwanza kama kaimu wa rais, Goodluck Jonathan ameongoza kikao cha baraza la mawaziri na kufanya mabadiliko katika baraza hilo.
Bwana Jonathan amemuondoa mamlakani mkuu wa sheria Michael Aondoakaa, na kumpa wadhifa wa mwingine serikalini.

Bwana Aondoakaa amekuwa akilaumiwa kwa kuzuia uchunguzi dhidi ya wanasiasa wanaokabiliwa na shutuma za ufisadi.

Bunge la Nigeria lilimkabidhi mamlaka mapema wiki hii. Amechukua nafasi ya Rais Umaru Yar'Adua, ambaye anaugua. Baraza la mawaziri limeridhia hatua hiyo, licha ya wasiwasi wa hapo awali kuhusu uhalali wake.

Afrika kusini yamuenzi Mandela


Raia wa Afrika Kusini leo wanaadhimisha miaka ishirini tangu alipoachiliwa huru Mzee Nelson Mandela.
Sherehe kubwa zitafanyika mjini Cape Town ambapo mke wa zamani wa Mandela, Winnie ataongoza maandamano hadi katika gereza ambalo alitumikia kifungo chake cha mwisho.

Mzee Mandela mwenye umri wa miaka 91 anatarajiwa kuonekana hadharani baada ya muda mrefu wakati atakapohudhuduria kwenye sherehe hizo ambapo Rais Jacob Zuma atahutubia taifa leo jioni.


Alitumikia kifungo kwa miaka 27 na baada ya kuachiliwa aliongoza mazungumzo yaliyosababisha kufanyika uchaguzi wa kwanza wa demokrasia. Katika uchaguzi huo Mzee Mandela alichaguliwa kuwa rais wa Kwanza mweusi nchini Afrika kusini mwaka wa 1994.

Mahakama ya London yakosolewa


Marekani inasema imesikitishwa sana na uamuzi wa mahakama ya london ambao umeilazimisha serikali ya Uingereza kufichua taarifa za kijasusi kuhusu kuteswa kwa raia wa Uingereza.
Raia huyo Binyam Mohammed, amesema alitishwa na kulazimishwa kutolala alipokuwa katika kizuizi cha Marekani nchini Pakistan.


Afisa mkuu wa Marekani amesema hatua hiyo itaathiri ushirikiano wa kijasusi kati ya Marekani na Uingereza.

Taarifa hizo zilitolewa na Idara ya ujasusi nchini Uingereza, MI5. Mahakama ya London ilisema taarifa hizo zilipaswa kufichuliwa kwa kuwa baadhi yazo tayari zilikuwa zimefichuliwa kwa umma nchini Marekani.

Haiti kuomboleza leo




Watu wa Haiti wametenga leo kama siku kuu ya kitaifa ya kuomboleza maelfu ya watu waliofariki katika tetemeko la ardhi lililotokea mwezi mmoja uliopita.
Ibada inatarajiwa kufanywa katikati mwa mji wa Port-au-Prince, ambako Ikulu ya Rais inaonekana ikiwa imeporomoka, kama mijengo mingine kote mjini. Serikali imepanga kuweka televisheni kubwa sehemu mbalimbali za mji ili watu wafuatilie kikamilifu ibada hiyo.

Tetemeko hilo lilisababisha vifo vya zaidi ya watu 230,000 na kuwaacha wengine zaidi ya milioni moja bila makaazi.

Clinton afanyiwa upasuaji wa moyo




Bill Clinton alilazwa hospitalini baada ya kulalamika kwamba ana maumivu ya kifua. Madaktari wanasema amewekewa mipira miwili katika mishipa yake ya moyo ambayo ilikuwa imeanza kuziba ili kuifungua.
Inaarifiwa kuwa rais huyo wa zamani wa Marekani yuko katika hali nzuri. Mke wake, Hillary ambaye ni waziri wa mambo ya nje wa Marekani amesafiri kwenda New York ili kuwa naye.

Bwana Clinton, aliwahi kufanyiwa upasuaji wa mishipa inayopeleka damu moyoni mwaka 2004.

Kwa miaka ya hivi majuzi, aliandamana na kumuunga mkono mkewe Hillary katika kampeni yake ya urais na tangu kutokea kwa tetemeko la ardhi nchini Haiti, Clinton amekuwa akihudumu kama mjumbe maalum wa umoja wa mataifa wa taifa hilo.

Uingereza na Rwanda kukabidhiana wafungwa




Makubaliano ya kukabidhiana wafungwa kati ya Rwanda na Uingereza yametiwa saini na waziri wa sheria wa Rwanda, Tharcis Karugarama na Balozi wa Uingereza nchini Rwanda, Nicolus Cannon Rwanda .
Makubaliano hayo yataruhusu watu waliohukumiwa na mahakama katika yoyote ya nchi hizo kutumikia kifungo nyumbani.

Rwanda ndiyo nchi ya pili ya kiafrika kutia saini makubaliano hayo na Uingereza, baada ya Uganda kusaini makubaliano kama hayo mwaka jana.

Wachambuzi wanasema Rwanda inataka kuonyesha jamii ya kimataifa kwamba inaweza kupokea watu waliohukumiwa na mahakama ya kimataifa ya Rwanda ambayo inasikiliza kesi za washukiwa wa mauaji ya kimbari ya mwaka 94.

Mahakama hiyo iliyo mjini Arusha, Tanzania, imekuwa ikikataa kuwakabidhi watu iliowahukumu kwa serikali ya Rwanda, ikidai kuwa mfumo wa gereza wa taifa hilo, hauwahakikishii haki wafungwa hao.

Togo yakata rufaa




Shirikisho la soka nchini Togo limekata rufaa katika mahakama ya usuluhishi ya mpira wa miguu (CAS) baada ya nchi hiyo kupigwa marufuku kushiriki mashindano mawili ya kombe la Afrika.
Adhabu hiyo ilitolewa baada ya Togo kujiondoa katika mashindano ya hivi karibuni nchini Angola.

Kujitoa kwao kulitokana na kushambuliwa na bunduki ambapo watu wawili wa timu ya Togo waliuawa.

Shirikisho la soka barani Afrika (caf) limesema, serikali iliingilia kati masuala ya soka kutokana na hatua ya waziri mkuu wa Togo kuitaka timu hiyo kurudi nyumbani.

Mkuu wa kamati ya mpito ya tume inayoshughulikia mpira Togo, Jenerali Seyi Memene amesema jopo la wanasheria wameteuliwa kuisimamia kesi hiyo.

Tuesday, February 9, 2010

Kisanduku cha ndege ya Ethiopia chapatikana




Vikosi vya uokozi nchini Lebanon vimefanikiwa kupata kisanduku cheusi kilichokuwa kikitumika kutunza kumbukumbu katika ndege ya shirika la ndege la Ethiopia iliyoanguka katika mwambao wa Mediterrania hivi karibuni, maafisa wanasema.
Ndege hiyo aina ya Boeing 737 ilianguka mnamo tarehe 25 Januari, muda mfupi baada ya kuruka kutoka uawanja wa ndege wa Beiruti wakati hali mbaya ya hali ya hewa, na kuwaua abiria wote 90 waliokuwemo katika ndege hiyo.

Afisa mmmoja wa jeshi amesema kisanduku hicho kimepelekwa katika kituo cha jeshi la wanamaji mjini Beiruti ili kukabidhiwa kwa wachunguzi wa ajali.

Kazi ya uokozi bado inaendelea kutafuta miili na kisanduku cha pili cha kumbukumbu katika eneo la ajali.

Waziri wa Usafirishaji nchini Lebanon Ghazi Aridi, alitangaza siku ya Jumamosi kuwa waokozi wamefanikiwa kugundua eneo viliko visanduku hivyo katika kina cha urefu wa mita 45 katika mwambao wa kijiji cha Naameh, karibu na kusini mwa uwanja wa ndege wa Beiruti.

Tokea wakati huo, waokozi wameweza pia kupata mabawa ya nyuma ya ndege hiyo na kazi imekuwa ikiendelea kuyaleta katika nchi kavu, afisa wa jeshi amesema.

Sababu ya ajali hiyo bado haijajulikana, hata hivyo maafisa wa Lebanon wamesema ndege hiyo haikufuata mwelekeo kama ilivyoelekezwa na kituo cha kuongoza ndege cha Beiruti wakati ikiruka.

Kisanduku hicho huenda kikaleta mwanga kujua ni kwanini rubani wa ndege hiyo alishindwa kufuata maelekezo aliyopewa wakati wa kurusha ndege, ingawaje alitambua maelekezo hayo.

Miili 15 imeopolewa kutoka katika ajali hiyo, lakini kwa mara kadhaa hali mbaya ya hewa imekuwa ikikwamisha zoezi la uokoaji katika kipindi cha wiki mbili zilizopita.

Benki ya Liechtenstein kuwalipa wakwepaji kodi hasara.


Benki ya Liechtenstein kuwalipa wakwepaji kodi hasara.

Vaduz, Leichtenstein.

Benki tanzu ya zamani ya benki ya LGT nchini Leichtenstein imeamuriwa kumlipa mkwepaji kodi wa Ujerumani euro milioni 7.3 katika hasara aliyopata . Mahakama nchini Leichtenstein imetoa hukumu kuwa benki hiyo ilichelewa kutoa taarifa kwa mteja wake kuwa data za mteja huyo zimeibiwa. Mdai amesema kuwa iwapo angearifiwa mapema, angeweza kuepuka faini ya euro milioni 7.3 inayotozwa kwa mkwepaji kodi. Mwajiriwa wa zamani wa benki aliiba na kuuza CD ambayo ina data za wateja kwa shirika la ujasusi la Ujerumani kwa kiasi cha euro milioni 4.5. Mmoja kati ya wakwepaji hao katika CD hiyo alikuwa mwenyekiti mtendaji wa huduma za posta nchini Ujerumani Klaus Zumwinkel.

Muasi wa Darfur hatoshtakiwa ICC




Majaji katika mahakama ya kimataifa ya kivita ya ICC wamefuta mashtaka dhidi ya kiongozi wa waasi katika jimbo la Darfur.
Bahr Idriss Abu Garda alishutumiwa kwa mauaji ya wanajeshi 12 wa kutafuta amani mwaka 2007. Alijisalimisha mwenyewe mwaka uliopita.

Lakini majaji walitoa uamuzi kuwa hakuna ushahidi wa kutosha kwa kesi dhidi yake.

Wiki iliopita,mahakama ya ICC ilisema mashtaka ya mauaji ya kimbari dhidi ya rais wa Sudan Omar al-Bashir yanaweza kuwasilishwa tena.Al-Bashir anatakiwa na mahakama hiyo kwa makosa ya kivita.

Wanajeshi 15 wa India wameuwawa mapema jana Jumatatu


Maporomoko ya barafu yaua 15 Kashmir

Kashmir.

Wanajeshi 15 wa India wameuwawa mapema jana Jumatatu wakati maporomoko makubwa ya barafu yalipofunika kituo cha mafunzo ya jeshi katika mji wa kitalii katika eneo linalodhibitiwa na India la Kashmir. Msemaji wa jeshi amesema kuwa maporomoko hayo yalikifunika kituo hicho cha jeshi kilichoko milimani kiasi saa tano asubuhi na kuporomoka na wanajeshi hao wakati wakiwa katika mafunzo. Watu 17 pia wamejeruhiwa katika maporomoko hayo ya barafu. Eneo hilo , liko katika urefu wa mita 2,730, ambapo ni katika mpaka unaogawanya Kashmir , kati ya India na Pakistan. Waokoaji bado wanawatafuta wanajeshi wawili zaidi ambao hawajulikani waliko na wanahofiwa wamezikwa chini ya barafu.

al-Shihri wa al-Qaeda alzishutumu Misr na Saudia.


al-Shihri wa al-Qaeda alzishutumu Misr na Saudia.

Sana'a.

Tawi la al-Qaeda nchini Yemen , kundi ambalo linadai kuhusika na jaribio lililoshindwa la kuilipua ndege ya shirika la ndege la Marekani siku ya Chrismass, limetoa wito wa mashambulio zaidi dhidi ya maslahi ya Marekani kila mahali. Katika ujumbe wa dakika 12 wa video uliotolewa katika mtandao wa internet, kiongozi wa pili wa al-Qaeda katika rasi ya Uarabuni, Said al-Shihri, pia ameishutumu Misr na Saudi Arabia kwa kusaidia kile alichosema kuwa ni Wakristo kupambana dhidi ya Uislamu katika rasi ya Uarabuni. Ameishutumu Saudi Arabia na Misr kwa kuhifadhi kile alichosema kuwa ni maslahi ya Wayahudi na Wakristo katika eneo hilo la rasi. Shihri, ambaye ni raia wa Saudi Arabia , alishikiliwa katika jela ya kijeshi la Marekani ya Guantanamo Bay, nchini Cuba, kwa muda wa karibu miaka sita.

Serikali ya mamlaka ya Palestina imetangaza kuwa inatarajia kufanya uchaguzi wa serikali za mitaa


Ramallah.

Serikali ya mamlaka ya Palestina imetangaza kuwa inatarajia kufanya uchaguzi wa serikali za mitaa katika ukingo wa magharibi na ukanda wa Gaza Julai 17. Chama cha Hamas kimejibu haraka kwa madai kuwa mamlaka ya Palestina haina haki ya kuitisha uchaguzi. Uchaguzi wa mwisho uliofanyika 2006 ulikipatia chama hicho chenye nadharia za kidini cha Hamas ushindi katika miji mingi mikubwa katika maeneo yote kabla ya kuchukua udhibiti kwa nguvu katika ukanda wa Gaza 2007.

Uchaguzi wa serikali za mitaa Palestinian Julai.

Rais wa Palestina Mahmoud Abbas , alipanga uchaguzi ufanyike mwezi uliopita kwa mujibu wa katiba, lakini baadaye alitangaza kuuahirisha hadi Juni mwaka huu. Chama cha Hamas katika ukanda wa Gaza kimesema kuwa hakutakuwa na uchaguzi kabla ya chama cha rais Mahmoud Abbas cha Fatah kufikia makubaliano ya maridhiano na chama hicho.

Mkuu wa zamani wa jeshi Sri Lankan akamatwa.


Mkuu wa zamani wa jeshi Sri Lankan akamatwa.

Colombo.

Mkuu wa zamani wa jeshi la Sri Lanka amekamatwa kwa kile kilichoelezwa kuwa ni kosa la kijeshi kwa mujibu wa msemaji wa jeshi hilo. Jenerali Sarath Fonseka aliongoza awamu ya mwisho ya operesheni ambayo ilisababisha kushindwa kwa uasi wa kundi la Tamil Tigers mwaka jana kabla ya kuingia katika kinyang'anyiro cha uchaguzi wa urais akishindana na rais Mahinda Rajapaksa mwezi uliopita. Tangu kuchaguliwa tena kwa Rajapaksa majeshi ya usalama yamekuwa yakiwakamata wafuasi wa Fonseka. Jenerali huyo wa zamani mwenye nyota nne amepinga matokeo ya uchaguzi wa rais akisema kuwa anania ya kupinga matokeo hayo katika mahakama kuu.

Jimmy Carter awasili nchini Sudan




Aliyekuwa rais wa Marekani Jimmy Carter amewasili nchini Sudan kwa mashauriano na rais wa nchi hiyo, Omar al-Bashir na maafisa wengine wakuu serikalini.
Carter anatarajiwa kuelezea wasi wasi wake kuhusu uchaguzi mkuu nchini humo unaopangwa kufanywa mwezi Aprili.

Bwana Carter pia anatarajiwa kushauriana na maafisa wa tume ya uchaguzi nchini humo. Mapema mwaka huu Bw. Carter alisema tume hiyo inakabiliwa na matatizo ya kifedha na haiungwi mkono ipasavyo na serikali ya nchi hiyo.

Ameelezea kusikitishwa kwake na kile anachosema ni usajili wa idadi ndogo ya wapiga kura na mapigano yanayoendelea katika eneo la darfur.

Wakfu wake, The Carter Center kwa sasa unatoa mafunzo kwa maafisa 3,000 watakaochunguza jinsi uchaguzi huo utakavyoendeshwa.

Uchaguzi ulikuwa wa haki; Wachunguzi




Kiev.

Nchini Ukraine, kiongozi wa upinzani Viktor Yanukovych ameibuka kuwa mshindi katika uchaguzi wa rais, akiendelea kuongoza kwa kiasi cha asilimia 3 wakati kiasi cha kura asilimia 99 zimekwisha hesabiwa. Wachunguzi wa kimataifa wameusifu uchaguzi huo kuwa ni huru na wa uaminifu, na kuimarisha madai ya ushindi ya Yanukovych na kumuacha waziri mkuu Yulia Tymoshenko akiwa amefungika kimkakati. Hata hivyo , waziri mkuu Tymoshenko bado anaendelea kuwa na wingi katika bunge la Ukraine, hali ambayo inaonekana kuendeleza mzozo katika utawala wa nchi hiyo.

Mbinyo wa kimataifa kwa ajili ya vikwazo vipya dhidi ya Iran umeongezeka


Vikwazo vikali zaidi.

Washington.

Mbinyo wa kimataifa kwa ajili ya vikwazo vipya dhidi ya Iran umeongezeka jana Jumatatu baada ya Iran kutangaza mipango ya kurutubisha kwa kiwango cha juu madini ya uranium na kuongeza maeneo mapya kumi ya kinuklia , na kuongeza hofu ya mataifa ya magharibi kuwa inataka kutengeneza bomu la kinuklia. Marekani na Ufaransa zimeongoza miito katika kile ambacho kinaweza kuwa sehemu ya nne ya vikwazo vikali zaidi, wakati wabunge waandamizi nchini Urusi, nchi ambayo hapo zamani ilikuwa inahimiza mazungumzo zaidi badala ya adhabu, imesema kuwa hatua za kiuchumi ni lazima zifikiriwe. Waziri wa ulinzi wa Marekani Robert Gates amesema kuwa maslahi ya Iran yatahifadhika iwapo haitakuwa na silaha za kinuklia.

Balozi wa Iran katika umoja wa mataifa mjini Vienna amekanusha madai kuwa jumuiya ya kimataifa inapaswa kuwa na hofu kuhusiana na urutubishaji huo wa kiwango cha juu wa madini ya uranium ambayo nchi yake inapanga kufanya.

Timu ya taifa Soka ya Benin yavunjwa


Shirikisho la mchezo wa soka nchini Benin, limevunja kikosi kizima cha timu ya taifa ya nchi hiyo kufuatia matokeo mabaya katika michuano ya kuwania kombe la mataifa bingwa barani Afrika.


Kocha wa timu hiyo raia wa Ufaransa Michel Dussuyer na maafisa wote wa kiufundi pia wamefutwa kazi. Kwa mujibu maafisa wakuu wa shirikisho hilo, kikosi hicho kimevunjwa kutokana na utovu wa nidhamu na kutowajibika kama wazalendo.

Timu hiyo inayojulikana kama The Squirrels, iliyaaga mashindano hayo nchini Angola, baada ya kumaliza katika nafasi ya tatu katika kundi lake na alama moja pekee

Daktari wa Michael Jackson, Conrad Murray alifikishwa katika mahakama mjini Los Angeles


Daktari wa Michael Jackson kizimbani

Daktari wa Michael Jackson, Conrad Murray alifikishwa katika mahakama mjini Los Angeles na kushtakiwa kwa kusababisha kifo cha mwanamuziki huyo miezi saba iliyopita.
Murray alikuwa ameajiriwa kumsaidia Michael Jackson kujiandaa kwa tamasha kadhaa mjini London na inaaminiwa kuwa alikuwa mtu wa mwisho kumwona mwanamuziki huyo akiwa hai.

Inadaiwa kuwa daktari Murray aliwaeleza wapepelezi kuwa alimpa Jackson dawa kadhaa ikiwemo ile yenye nguvu nyingi ya Propofol ambayo kwa kawaida hutumika hospitalini pekee.

Inadaiwa baada ya kumpa dawa hiyo Murray aliondoka kwa muda mfupi kutoka chumbani mwa Jackson ili kupokea simu na aliporudi akampata mwanamuziki huyo hapumui.

Afisa wa upelelezi alimpata daktari huyo na hatia ya kumpa Michael Jackson propofol kwa kupita kiasi kilichostahili na hivyo kusababisha kifo chake. Lakini alipofikishwa mahakamani kwa kosa hilo ambalo linaweza kumpa kifungo cha miaka 4 gerezani, Daktari Murray alisisitiza kuwa hakuna na hatia.

Daktari Murray aliachiliwa kwa dhamana ya dola 75,000 akisubiri kusikilizwa kwa kesi yake mwezi april

Saturday, February 6, 2010

Terry ang'olewa unahodha England




John Terry amevuliwa unahodha wa timu ya taifa ya England kutokana na madai ya kuwa na uhusiano wa kimapenzi na mpenzi wa mchezaji mwenzake.
Terry, mwenye umri wa mika 29, kabla ya uamuzi huo alifanya mazungumzo na kocha Fabio Capello wa England katika uwanja wa Wembley siku ya Ijumaa.

"Baada ya kutafakari kwa muda mrefu, nimeamua kwamba litakuwa jambo jema kwangu kumvua John Terry unahodha," alieleza Capello katika taarifa.

Terry mlinzi wa Chelsea ambaye amerithiwa wadhifa huo na mlinzi mwenzake Rio Ferdinand, alisema anaheshimu uamuzi wa Capello kumng'oa yeye.

Matokeo ya Ligi Kuu England

Matokeo ya baadhi ya mechi za ligi kuu ya England zilizochezwa siku ya Jumamosi 06/02/2010 ni kama ifwatavyo:
Bolton 0-0 Fulham

Burnley 2-1 West Ham

Hull 2-1 Man City

Liverpool 1-0 Everton

Man Utd 5-0 Portsmouth

Stoke 3-0 Blackburn

Sunderland 1-1 Wigan

Shangaziye Obama ajitetea mahakamani


Shangaziye Rais Barrack Obama, Zeituni Onyango amefika mbele ya mahakama moja mjini Massachussets, katika jaribio lake la pili, la kutafuta hifadhi ya kisiasa nchini Marekani.

Wakili wake amesema kesi ya Bi Onyango inazingatia misingi ya afya yake na hofu ya mapigano ya kikabila nchini Kenya. Bi Zietuni Onyango alijitetea faraghani.

Madaktari wawili pia walitoa ushahidi kwa niaba yake. Afisa wa idara ya habari katika Ikulu ya White House amesema Rais Obama, hajazungumza na shangaziye, tangu hatma yake ilipojulikana kabla ya kufanyika kwa uchaguzi wa urais.

Uchaguzi wa Gavana kufanyika Anambra, Nigeria




Hali ya Ulinzi imeimarishwa katika jimbo la kusini mashariki la Anambra nchini Nigeria, siku moja kabla ya kufanyika uchaguzi wa gavana wa eneo hilo.
Waandishi wa Habari wanasema kuna hali ya wasi wasi kuhusu unachaguzi huo, unaoendeshwa na tume ya uchaguzi iliyosimamia uchaguzi mkuu wa mwaka wa 2007, ambao ulighubikwa na wizi wa kura na udanganyifu.

Miongoni mwa masuala yanayozua utata ni pamoja na usajili wa wapiga. Wachunguzi wanasema matokeo ya uchaguzi huo wa Anambra, huenda utakatoa mwelekeo kuhusu shughuli za uchaguzi nchini humo miaka ijayo.

Wamishonari mahakamani Haiti




Wamishonari kumi raia wa marekani wamefikishwa mahakamani kwa madai ya kuwateka nyara watato nchini Haiti.
Raia hao walishtakiwa kwa kujaribu kuwasafirisha watoto nje ya nchi hiyo baada ya tetemeko kubwa la ardhi katika mji mkuu wa Port-Au_Prince.

Wengi wao walifunika nyuso zao na kuimba nyimbo za kidini wakati walipokuwa wakiondolewa mahakamani.

Washukiwa hao wanadai kuwa walikuwa wakiwapeleka watoto hao katika makao moja ya watoto ilioko nchi jirani ya Jamhuri ya Dominican.