KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Friday, December 10, 2010

Wazazi watozwa Sh20,000 kuandikisha watoto la kwanza


Hamad Amour (TSJ)
KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida, baadhi ya shule za msingi jijini Dar es Salaam zinawatoza wazazi kati ya Sh7,000 na Sh20,000 kuwaandikisha watoto darasa la kwanza.

Malipo hayo ni kinyume na agizo lililotolewa serikali kuwa watoto wanaonza darasa la kwanza waandikishwe bure ili kufikia malengo ya Milenia ya kuhakikisha kuwa watoto wote wenye umri wa miaka saba wanaanza elimu ya msingi.

"Uandikishaji wanafunzi darasa la kwanza ufanyike bure," ilisema sehemu ya waraka uliotolewa Oktoba 28, mwaka huu na Ofisa Elimu wa Manispaa ya Temeke kwenda kwa wakuu wa shule katika manispaa hiyo.

Waraka huo namba saba wa mwaka 2001 wenye kumbukumbu namba TMC/De/T.I/Vol 11/100 uliotolewa kutekeleza maagizo ya Serikali Kuu kuzuia michango mashuleni, ulitaka wanafunzi wote wenye umri wa kuanza darasa la kwanza waandikishwe bure.

Uchunguzi wa gazeti hili katika shule za msingi Kingugi, Annex na Kizinga za jijini Dar es Salaam zimeendelea kuwatoza wazazi wazazi fedha wakati wa kuandikisha watoto wa darasa la kwanza.

Tatizo lingine linaloambatana na michango hiyo ni risiti zinazotolewa kutolingana na viwango vya malipo, jambo ambalo linadhihisha kuwa wazazi hao wanaibiwa.

Mmoja wa wazazi walioenda kuandikisha watoto katika Shule ya Msingi Kingungi ambaye hakutaka atajwe gazetini alilalamikia michango hiyo na kueleza kuwa hana uwezo wa kupata Sh 7,200 alizotakiwa kulipa.

Mzazi huyo ambaye mwandishi wa habari hii alilazimika kumchangia Sh2,200 ili akamilishe malipo hayo, alisema malipo hayo ni kinyume na taratibu.

"Mimi uwezo wa kuchangia Sh7,200 sina, mume wangu ni mzee na hatuna kipato chochote cha maana," alisema.

Katika Shule ya Msingi Anex iliyoko Mbagala, jijini Dar es Salaam habari zimeeleza kuwa wanafunzi wanaandikishwa baada ya kulipa Sh19,500.

Mwalimu Mkuu wa Shule hiyo hakupatikana kuzungumzia suala hilo lakini Mwalimu wa Taaluma shuleni hapo ambaye alikataa kutaja jina lake alifafanua kuwa shule hiyo inatoza Sh2,400 tu za ulinzi kwa mwaka.

Lakini nyaraka zilizopatikana shuleni hapo zimeonyesha kuwa wanatoza fedha nyingi na kati ya hizo, Sh 10,000 zinatumika kujenga uzio, Sh5,000 manunuzi ya fulana, Sh 1,300 mchango wa mshahara wa mlinzi kwa mwaka na Sh1,000 kwa ajili ya nembo ya shule.

"Malipo hayo yote yalitafanyika Desemba 8, 2010, saa 3 asubuhi," imesema sehemu ya waaraka huo ambao Mwananchi inao

Katika Shule ya Msingi Kizinga, wanafunzi wanachangishwa Sh7,000 kwa ajili ya ulinzi, fulana na nembo.

Hata hivyo, Mkuu wa Shule hiyo, Ephrahim Killaha alieleza kuwa mchango huo ni wa hiari na kwamba mwanafunzi hafukuzwi shule kwa kushindwa kulipa.

Mbunge wa Jimbo la Kigamboni, Dk Fustine Ndugulile alisema ana taarifa na michango hiyo na kwamba tayari amewasiliana na Mkurugenzi na Ofisa Elimu wa Manispaa ya Temeke, lakini wote wamekana kutoa agizo hilo.

"Wazazi wote wanaokwenda kuandikisha watoto wa darasa la kwanza katika shule yoyote, waki daiwa fedha wambie mwalimu awape waraka unaompasa afanye hivyo vinginevyo michango hiyo sio halali," alisema Dk Ndugulile.


Afisa Uhusiano wa Halmashauri ya Manispaa ya Temeke, Lynn Chawala alisema hana taarifa za michango hiyo ila akaeleza kuwa ni makosa kumtoza mwanafunzi ambaye hajaanza masomo.

“Sina taarifa hizo lakini utaratibu ni kwamba wanafunzi wote waandikishwe bure,” alisema Chawala.

Chawala aliahidi kufuatilia suala hilo na kulitolea ufafanuzi baada ya kuwasiliana na wahusika

No comments:

Post a Comment