KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Tuesday, December 14, 2010

IRAN KUSHIKA UZI ULE ULE



Großansicht des Bildes mit der Bildunterschrift: Waziri wa mambo ya nje wa Iran M Mottaki amefukuzwa.Iran yasema sera zake hazitabadilika licha ya waziri Mottaki kufukuzwa.

Iran imesema leo sera zake hazitaathirika baada ya waziri wa mambo ya nje Manoucher Mottaki kufukuzwa kazi jana.

Msemaji wa wizara ya mambo nje ya Iran amehakikisha kuwa hakuna kitakachobadilika.Msemaji huyo Ramin Mehmanparast ameeleza kuwa hapatakuwa na mabidiliko pia kuhusu mazungumzo juu ya mpango wa nyuklia wa Iran.

Amesema wizara ya mambo ya nje ya Iran inazitekeleza sera zilizoamuliwa na viongozi wa ngazi za juu.Bwana Ramin Mehmanparast amefafanua kuwa sera muhimu za kimataifa za Iran zinaamuliwa na viongozi wa ngazi za juu.Amesema hafikiri iwapo watu wataona mabadiliko katika sera za msingi za Iran.

Rais Mohmoud Ahmadinejad jana alimfukuza kazi waziri wake wa mambo ya nje Manouchehr Mottaki na kumteua Ali Akbar Salehi kuushika wadhifa huo kwa muda.Bwana Ali Akbar Salehi ni mkuu wa shirika la nishati ya nyuklia la Iran na pia ni makamu wa rais.

Hakuna sababu zilizotolewa juu ya hatua hiyo ya kushangaza iliyochukuliwa na rais Ahmadinejad, siku chache tu baada ya Iran kushiriki katika mazungumzo muhimu juu ya mpango wake wa nyuklia na wajumbe wa mataifa makubwa yaliyofanyika mjini Geneva mapema mwezi huu. Mazungumzo zaidi yamepangwa kufanyika mwezi ujao nchini Uturuki.

Akizungumza juu ya hatua ya Rais Ahmadinejad ya kumfukuza Mottaki,waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Guido Westerwelle amesema ,licha ya hatua hiyo anatumai kuwa mazungumzo na Iran yataendelea kufanyika.

Amesema Ujerumani inataraji kuwa mazungumzo yaliyoanza hivi punde tu mjini Geneva yataendelea. Waziri Westerwelle amesema lazima mazungumzo yaendelee kufanyika katika hali yoyote ile.

Kwenye mkutano juu ya masuala ya usalama uliofanyika Bahrain mapema mwezi huu, waziri aliefukuzwa bwana Mottaki aliisifu kauli iliyotolewa na waziri wa mambo ya nje wa Marekani Hillary Clinton kwamba Iran inayo haki ya kuwa na mpango wa nishati ya nyuklia kwa madhumuni ya amani.

Waziri Clinton aliliambia shirika la Utangazaji la Uingereza BBC kwamba Iran inaweza kurutubisha madini ya uranium kwa madhumuni ya mani katika siku za usoni mradi tu nchi hiyo inayafanya hayo katika njia ya kuwajibika.

Kauli ya bwana Mottaki ilionekana kuenda kinyume na msimamo rasmi wa serikali ya Iran kwamba mpango wake wa kurutubisha madini ya uranium siyo suala la kuzungumziwa.

Mwandishi/Mtullya abdu/AFPE/ZAR.

Mhariri/Mohammed Abdul-Rahman

No comments:

Post a Comment