KARIBU MAISHANI

KARIBU MAISHANI

Monday, May 10, 2010

Chelsea mabingwa Ligi Kuu ya England 2010


Chelsea wamemaliza msimu kwa kishindi kizito wakati walipoichapa Wigan magoli 8 - 0 katika mojawapo ya mechi 10 za kukamilisha msimu zilizochezwa Jumapili. Ingawa Manchester United walipata kazi rahisi kuitandika Stoke City 4 - 0, Chelsea wamefikisha pointi 86 na Manchester United wana pointi 85.

Nicholas Anelka ndiye aliwafungia Chelsea goli la kwanza kunako dakika ya tano ya mchezo alipomalizia mpira wa adhabu uliopigwa na Didier Drogba.

Goli la Anelka lilifungua mwanya kwa Frank Lampard kupachika mkwaju wa penati baada ya kufanyiwa madhambi na Gary Caldwell, ambaye alitolewa nje kwa kadi nyekundu.

Salomon Kalou alitumbukiza la tatu baada ya mapumziko baada ya kugongeana vizuri na Lampard na Anelka akaandika la nne.

Karamu ya magoli ilikuwa inazidi kushika kasi, Didier Drogba alianza pole pole lakini hatimaye alifunga matatu na kumaliza msimu akiwa mfungaji bora.

Kwanza alifungwa kwa kichwa, kisha mkwaju wa penati na goli la ndani ya 18. Mwishowe Ashley Cole akamalizia la mwisho.

No comments:

Post a Comment